SAA chache baada ya Rais Kikwete kutangaza Baraza jipya, baadhi ya wabunge wametoa maoni wakiunga mkono na wengine wakipinga uteuzi huo.
Baadhi walishauri kuchukuliwa hatua za kisheria dhidi ya mawaziri
waliobaki na waliong’olewa madarakani ambao taarifa ya Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliwataja kuhusika na
ubadhirifu.
Mbunge wa Kasulu Kusini, David Kafulila, alieleza kufurahishwa kwake
na Rais kubadilisha mawaziri na kuondoa watuhumiwa wakuu, lakini
hakupenda kuona wengine walionyooshewa vidole na wabunge kwa ubadhirifu
wakiachwa.
“Sijaridhishwa na mpangilio wa baadhi ya mawaziri. Kuachwa kwa
Mkuchika nako ni tatizo kwa sababu alikotoka aliharibu. Mtu kama January
Makamba angepelekwa Madini na Masele angekuwa Mawasiliano, Sayansi na
Teknolojia. Mpango huo angalau ungesaidia wananchi kimaendeleo”.
Kafulila alipinga kuundwa kwa wizara isiyo maalumu kwa maelezo kuwa
imelenga kuongeza gharama. Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe alipinga
kuachwa kwa Mkuchika.
“Huyu ameboronga Tamisemi na leo anapelekwa Utawala Bora ataweza
nini? Naheshimu uteuzi wa Rais lakini kwa kurudisha waliotuhumiwa kwa
ubadhirifu na utendaji mbovu simuungi mkono na sifurahii”.
Akizungumzia kuondolewa kwa Mkullo, Filikunjombe alisema hiyo ni faraja ya kila Mtanzania.
“Niko safarini na sijasikiliza uteuzi, lakini nimepata taarifa
kuhusu kuendelea kwa mawaziri waliopigiwa kelele kama vile Mkuchika,
hapo kuna tatizo”.
Mbunge wa Mbozi Mashariki, Geodfrey Zambi, alieleza kufurahishwa na
uteuzi huo ingawa alinung’unikia kuendelea kwa baadhi ya mawaziri
waliokuwa wamelalamikiwa na wabunge.
“Rais amefanya mabadiliko, sipingani naye kwa sababu ameangalia msingi unaotakiwa kuwa anaoteua ni wabunge.
Alioona wanamfaa amewapa nafasi. Huo ni uamuzi wake siupingi,
lakini nimesikitika kuona baadhi ya waliolalamikiwa wamo bado, hatuna
cha kufanya zaidi ya kuwapa nafasi wafanye kazi,” alisema Zambi..
Rais Kikwete alisema kuanzia sasa Waziri atawajibika kisiasa pamoja
na wote waliosababisha afikie hatua hiyo. Alisema baadhi ya viongozi
wamekuwa wakilazimika kuwajibika hata kwa makosa yaliyofanywa na
wengine, hivyo kuponzwa.
“Ndiyo, Waziri atawajibika kisiasa, lakini aliyesababisha Waziri
awajibishwe naye hataachwa. Kama ni shirika, Ofisa Mtendaji Mkuu
ataondoka na Bodi itaondoka pamoja na watendaji wakuu wa shirika au
wizara,” alisema Rais.
Aliongeza kuwa katika baadhi ya maeneo, watu wamekuwa akifanya fitna
ili Waziri aondoke kwa kuwajibika, wakisema walikuja wengi wakaondoka
na yeye ataondoka, hivyo kuanzia sasa hilo halitakubalika.
Kuhusu ushauri wa kuigawa Wizara ya Nishati na Madini, alisema ni
wazo zuri lakini alishauriwa kuwa kuunda Wizara mpya hivi sasa wakati
Bajeti ilishapita ni kutafuta mzigo.
Hivyo alisema anaiacha ilivyo hadi siku zijazo kama watakaokuwapo
wataona inafaa wafanye hivyo, lakini akaamua iwe na naibu mawaziri
wawili mmoja ashughulike kwa kina na madini na mwingine nishati.
HABARILEO
No comments:
Post a Comment