Monday, July 30, 2012

Maoni ya John Mnyika (Mb) baada ya Spika kuvunja Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini

Kufuatia uamuzi wa Spika wa Bunge jana jumamosi tarehe 28 Julai 2012 kukubali kuvunja Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini nimetakiwa kutoa maoni yangu kuhusu uamuzi husika kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini na mbunge: Kwa maoni yangu uamuzi huo ni sahihi lakini umechelewa na pekee hauwezi kurejesha heshima ya bunge kwa ukamilifu wala hautaweza kushughulikia uzembe na udhaifu ulioko kwenye bunge na kwenye serikali ikiwa hautaambana na hatua nyingine za ziada na za haraka.Kwa upande mwingine, uamuzi huo umedhihirisha nilichokisema kwa nyakati mbalimbali kuhusu uzembe wa kibunge pamoja na udhaifu wa serikali.

Ukiondoa tuhuma za wabunge wanaodaiwa kupokea rushwa ama kuwa na maslahi ya kifedha kwenye wizara, taasisi au mashirika wanayoyasimamia kwenye kamati mbalimbali, heshima ya bunge imeathiriwa vile vile na maamuzi mathalani uamuzi wa kuchaguliwa kwa mtuhumiwa wa ufisadi wa Rada Mbunge Andrew Chenge kuwa mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi.

Hivyo hatua zaidi zichukuliwe ikiwa ni pamoja na kuvunja na kamati zenye wajumbe waliotuhumiwa na pia kufanya mabadiliko makubwa kwenye wajumbe wa kamati mbalimbali za kudumu za bunge ili kupunguza maslahi ya kifedha ama tuhuma za rushwa miongoni mwa wajumbe wa kamati. Aidha Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge imalize kazi yake kwa dharura ili majina ya wahusika yatajwe ndani ya bunge na bunge lijadili kupitisha maazimio ya hatua za ziada za kuchukuliwa na vyombo huru vya kiuchunguzi na hatimaye watakaothibitika kuvunja sheria wafikishwe mahakamani. Pamoja na hatua hizo, Kamati za Vyama nazo zichukue hatua kwa wabunge wake watakaotajwa ili kudumisha misingi ya uadilifu na uwajibikaji kwa maslahi ya umma.
Hata baada ya hatua hizo, izingatiwe kuwa Bunge litaweza kujinasua kwenye uzembe ikiwa litatimiza kikamilifu wajibu wake wa kuisimamia serikali kwa mujibu wa ibara ya 63 kuondoa udhaifu wa serikali kwenye sekta ya nishati na sekta nyingine muhimu za taifa kwa kuhakikisha maazimio yote ya bunge yanatekelezwa kwa ukamilifu na kwa haraka kama nilivyoeleza kwenye maoni ya kambi rasmi ya upinzani bungeni tarehe 15 Julai 2011 na tarehe 27 Julai 2012.

Nilisema bungeni kwamba “Naamini iwapo maazimio ya Bunge juu ya Mkataba baina ya TANESCO na Kampuni ya Richmond Development Company LLC yangetekelezwa yote na kwa wakati toka mwaka 2008, maazimio ya bunge juu ya uendeshaji wa sekta ndogo ya gesi asili ya mwaka 2011 yangezingatiwa yote na kwa haraka, maazimio kuhusu uhalali wa utaratibu wa Wizara ya Nishati na Madini kuchangisha fedha kwa ajili ya kupitisha bajeti bungeni ya mwaka 2011 yangechukuliwa kwa uzito unaostahili; taifa lingeepushwa kurudia mijadala ile ile kuhusu Wizara hii hii mara kwa mara”.

Mathalani, Waziri wa Nishati na Madini ameeleza bungeni tarehe 28 Julai 2012 kuwa wapo wabunge wanaotuhumiwa kufanya biashara zenye kulihujumu Shirika la Umeme (TANESCO) na Spika wa Bunge akahitimisha kuwa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge itachunguza tuhuma husika na pia kwamba inakusudiwa kutungwa kwa Kanuni za Maadili (Code of Conduct) ili kudhibiti hali hiyo.

Hata hivyo, Serikali na Uongozi wa Bunge kwa pamoja wamesahau kuwa mwaka 2008 baada ya Kashfa ya Richmond iliazimiwa katika Azimio Na. 11, kwamba “Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya Mwaka 1995 (The Public Leadership Code of Ethics Act), ifanyiwe marekebisho makubwa ili kudhibiti utaratibu unaoonekana wa kawaida sasa wa Viongozi Waandamizi wenye dhamana ya kisiasa kuendelea na biashara zao binafsi wakiwa madarakani, jambo ambalo lina mgongano wa kimaslahi. Serikali ianze rasmi maandalizi ya majadiliano ya kina kuhusu suala hili ndani na nje ya Bunge kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali.”

Bunge lilitaarifiwa Februari 2010 kuhusu utekelezaji wa Serikali kwamba kikundi kazi (Task Force) kiliundwa ambacho kiliandaa waraka wenye mapendekezo ya kurekebisha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, (Sura 398) ambao ulikuwa katika ngazi ya kujadiliwa na Kamati ya Makatibu Wakuu (IMTC). Aidha, Bunge lilielezwa kuwa serikali ilitarajia kuwasilisha muswada husika katika mkutano wa kumi na tisa wa Bunge la tisa. Muswada huo haukupitishwa katika Bunge la tisa kama ilivyoshauriwa na kamati na mpaka kutokana na uzembe na udhaifu azimio hilo halijatekelezwa na tuhuma nyingine zimeendelea kuibuka.

Aidha, kumetolewa madai ya baadhi ya wabunge kupokea ama kudai rushwa suala ambalo nalo Spika wa Bunge ametoa uamuzi kuwa litashughulikiwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge. Lakini Serikali na Uongozi wa Bunge kwa pamoja wamesahau kwamba hii si mara ya kwanza kwa tuhuma za namna hiyo kutolewa juu ya baadhi ya wabunge wa kamati mbalimbali za bunge.

Hata hivyo, kwa sababu ya kutochukua hatua kwa haraka na kwa ukamilifu tuhuma kama hizo zitaendelea kujirudia hata baada ya kuvunjwa kwa kamati ya bunge ya nishati na madini. Izingatiwe kwamba madai ya rushwa kutolewa kwa wabunge yaliwahi kujitokeza kuhusu Kamati ya Nishati na Madini na binafsi nilitoa ushuhuda kwa Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mwaka 2011, na nikatoa ushuhuda tena kwa Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza uhalali wa utaratibu wa Wizara ya Nishati na Madini kuchangisha fedha kwa ajili ya kupitisha bajeti bungeni mwaka 2011 kuwa yamekuwepo matukio ya kushawishi wabunge kwa rushwa hata hivyo hatua hazikuchukuliwa ama kuvunja kamati zilizotajwa au kuwachukulia hatua wahusika.

Suala hili likatajwa tena na Mbunge wa Kigoma Kaskazini David Kafulila kuhusu Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa na likatajwa tena na Kiongozi wa Upinzani Freeman Mbowe na Mbunge wa Kyela Dr Harrison Mwakyembe kuhusu uchaguzi wa Afrika Mashariki lakini hatua hazikuchukuliwa kuchunguza wabunge husika na kuchukua hatua. Iwapo maazimio kuhusu uhalali wa utaratibu wa Wizara ya Nishati na Madini kuchangisha fedha kwa ajili ya kupitisha bajeti bungeni ya mwaka 2011 (Maarufu kama Sakata la Jairo), yangetekelezwa na wahusika wangechukuliwa hatua ingejenga nidhamu pia kwa watendaji wa wizara na mashirika ya umma kuhusu rushwa na matumizi mabaya ya fedha za umma yenye kulenga kuwaathiri wabunge kwa rushwa na maslahi mengine ya kifedha.

Katika hali inayoonyeha kwamba Serikali bado haioni uharaka na ulazima wa kuchukua hatua, wakati bunge lilipokaa kama kamati tarehe 28 Julai 2012 kupitisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini nilitaka ufafanuzi kutoka kwa Waziri wa Nishati na Madini kuhusu utekelezaji wa maazimio hayo ambayo mpaka sasa hakuna taarifa ya utekelezaji iliyowasilishwa bungeni toka yapitishwe mwezi Novemba mwaka 2011; lakini Waziri akajibu tu kwamba hawezi kufanyia kazi taarifa za magazetini, bila kujali kwamba nilichouliza hakihusu taarifa za magazetini bali maazimio ya bunge baada ya kazi iliyofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na ikarudiwa tena na Kamati Teule ya Bunge ambayo ilihoji wahusika na kupata pia vielelezo.

Kwa hiyo, ni muhimu Serikali na Uongozi wa Bunge ukarejea kwenye Hotuba niliyowasilisha bungeni na kuchukua hatua kwa usimamizi wa Rais, Waziri Mkuu na Spika wa Bunge juu ya masuala yote niliyoyaeleza. Pamoja na kutaja ushawishi uliokuwa ukifanywa kwa wabunge kuhusu suala la ununuzi wa mafuta ya IPTL, na ufisadi ndani ya TANESCO nilieleza pia masuala mengine makubwa kwenye nishati na madini yenye kuhusu mabilioni ya shilingi kwenye mikataba mikubwa ya umeme, madini, mafuta na gesi asili pamoja na hatua za mabadiliko ya kimfumo zinazopaswa kuchukuliwa.

Nimetoa maoni haya leo, Jumapili tarehe 29 Julai 2012:

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini

Serikali ya Tanzania yalifungia gazeti la MwanaHalisi

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imelifungia gazeti la MwanaHalisi kwa muda usiojulikana kwa kile kilichoelezwa kuwa na mwenendo wa kuandika habari na makala za uchozezi.

Sababu nyingine ya kufungiwa kwa gazeti hilo ni pamoja na kujenga uhasama na uzushi likiwa na nia ya kusababisha wananchi kukosa imani na vyombo vya dola hali inayoweza kuhatarisha amani na mshikamano wa nchi. 

Akisoma tamko la Serikali leo jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Wizara ya Habari (MAELEZO), Phabian Lugaikamu, alisema kuwa katika toleo la gazeti hilo namba 302, 303 na 304 ya mwaka 2012 na mengine yaliyotangulia yalichapisha habari na makala zenye kueneza na kujenga hofu kwa jamii. '

“Mhariri wa gazeti la Mwanahalisi ameitwa na kuonywa mara nyingi lakini hataki kukiri kuwa maudhui ya makala zake hazina tija kwa jamii,pia hazifuati weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari” alisema.

Aidha, alisema kuwa mhariri huyo mara zote katika utetezi wake amekuwa akinukuu kifungu cha 18 cha katiba ya nchi kinachotoa uhuru wa kutoa maoni na kwa makusudi kutokunukuu kifungu ca 30 cha katiba hiyo kinachoweka ukomo wa uhuru.

“Serikali imeamua kulifungia gazeti hilo kutochapishwa kwa muda usiojulika kwa mujibu wa sheria ya magazeti ya mwaka 1976, kifungu namba 25(i), adhabu hiyo itaanza tarehe 30 Julai, 2012 kwa mujibu wa tangazo la serikali namba 258 lililochapishwa katika gazeti la Serikali na kutolewa jijini Dra es Salaam Julai 27, 2012” alisema.

---
habari via Francis Dande/Habari Msego blog


TAMKO LA SERIKALI LA KULIFUNGIA GAZETI LA MWANAHALISI


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imelifungia kutochapishwa gazeti la MwanaHalisi kuanzia 30 Julai, 2012 kwa muda usiojulikana kutokana na mwenendo wake wa kuandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi likiwa na nia ya kusababisha wananchi kukosa imani na vyombo vya dola hali inayoweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

Katika matoleo yake hivi karibuni, gazeti la MwanaHalisi toleo Na. 302 la Jumatano Julai, 11 – 18, 2012 na toleo Na. 303 la Jumatano Julai 18 – 24, 2012 na toleo Na. 304 la Jumatano Julai 25 hadi 01 Agosti, 2012 na mengine yaliyotangulia yamekuwa yakichapisha habari na makala zenye kueneza na kujenga hofu kwa jamii. Mhariri wa gazeti la MwanaHalisi, ameitwa na kuonywa mara nyingi, lakini hataki kukiri kuwa maudhui ya makala zake hazina tija kwa jamii, pia hazifuati weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

Mhariri, mara zote katika utetezi wake amekuwa akinukuu kifungu cha 18 cha Katiba ya nchi yetu ambacho kinatoa uhuru wa kutoa maoni na kwa makusudi kutonukuu kifungu cha 30 cha Katiba hiyo kinachoweka ukomo wa uhuru.

Uamuzi wa Serikali

Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i), adhabu hiyo itaanza tarehe 30 Julai, 2012 kwa mujibu wa Tangazo la Serikali (Government Notice) Na. 258 lililochapishwa katika Gazeti la Serikali na kutolewa jijini Dar Es Salaam tarehe 27 Julai, 2012.

Serikali inawataka wamiliki, wahariri na wanahabari kuzingatia sheria, uzalendo, weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari katika kutekeleza wajibu wa kuhabarisha, kuelimisha na kutoa burudani kwa wananchi.

Kama ilivyoelezwa Bungeni wakati wa kuwasilisha Bajeti ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo hivi karibuni waandishi na watangazaji wa habari wanatakiwa kuhakikisha kuwa habari wanazoziandika na vipindi wanavyoandaa vinazingatia taaluma na kuweka mbele maslahi ya Taifa letu na uzalendo. Uhuru na haki ya vyombo vya habari uendane na wajibu.

Kuanzia sasa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya vyombo vya habari ambavyo kwa maksudi vitatoa taarifa za uchochezi ambazo zitahatarisha hali ya amani na utulivu uliopo nchini mwetu.

Imetolewa na OFISI YA MSAJILI WA MAGAZETI
WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO
30 Julai, 2012

Sunday, July 29, 2012

Wabunge watano (3 CCM, 2 Upinzani) wametajwa kuhusika na ufisadi wa TANESCO

WAKATI wabunge wakitoa tuhuma nzito dhidi ya wenzao wanaodaiwa kujihusisha na ufisadi ndani ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), imebainishwa kuwa wabunge wenye tabia hiyo ni watano, watatu kutoka chama tawala CCM na wawili upinzani.

Habari zilizopatikana jana mjini Dodoma zimeeleza kuwa baadhi ya wabunge hao wanatoka katika Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, huku wengine wakitoka Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, wabunge hao wamedaiwa kuwa wamekuwa wakitumia nafasi zao za ubunge na ujumbe wa kamati kufanya biashara na TANESCO na kutetea mafisadi ndani ya shirika hilo la umma.

Gazeti hili (MWANANCHI) limefanikiwa kupata majina ya wabunge hao, ambayo leo hatutayataja kwa sababu za kitaaluma.

Baadhi ya wabunge waliochangia hoja hiyo bungeni juzi na jana walisema kuwa, wanawafahamu wabunge hao kwa majina, lakini hawapendi kuwataja kwa kuwa siyo wakati mwafaka.

Moto wa kutaka kutajwa kwa majina ya wabunge hao ulikolezwa jana na Mbunge Vita Kawawa wa Namtumbo (CCM) aliyeomba Mwongozo wa Spika, akitaka jambo hili lijadiliwe na Bunge na kupendekeza kuwa, Kamati za Bunge zinazotuhumiwa kwa rushwa zivunjwe,  “Waheshimiwa wabunge wamejadili suala hili kwenye wizara, lakini kwa mujibu wa kifungu cha 55 (3)f  mbunge au waziri anaweza kutoa hoja ili jambo fulani lijadiliwe. Sasa naomba kutoa hoja ya kujadili suala hilo," Kawawa alisema.

Aliliomba pia Bunge likubali kuivunja na kuiunda upya Kamati ya Nishati na Madini na kamati nyingine zilizolalamikiwa kwa rushwa. Hoja hiyo iliungwa mkono na wabunge.

Baada ya hoja hiyo kuungwa mkono Spika wa Bunge, Anne Makinda alisimama na kukubali hoja hiyo ya Kawawa na kutangaza kuivunja Kamati ya Nishati na Madini.

Spika Makinda alisema ameiagiza Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge kutengeneza kanuni za kuwadhibiti wabunge wenye tabia hiyo ya kupokea rushwa kutoka kwa watu mbalimbali ili kutimiza matakwa yao binafsi.

"Ninakubali kuivunja Kamati ya Nishati na Madini na zingine ambazo zitatajwa kwenye tuhuma hizo. Nalipeleka pia suala hilo kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, halafu kama ni kutajwa (wabunge hao), basi tutapata mwongozo wa kamati hiyo." alisema Spika Makinda na kuongeza: "Nasema kwa dhati kabisa, kitendo hiki hakikubaliki ndani ya Bunge hili. Wabunge mkae vizuri. Kama kuna baadhi yetu wanaenda huku na huku kujitafutia masilahi binafsi, tutawezaje kuisimamia Serikali?"

Selemani Zedi

Baada ya Spika kutangaza kuvunja Kamati ya Nishati na Madini, Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Seleman Zedi alisema kuwa ameshtushwa na uamuzi huo na anasubiri uamuzi wa Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge, "Nimeshtushwa sana na uamuzi huo, lakini tusubiri Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge," alisema Zedi.

Waziri Prof. Muhongo

Akihitimisha hoja ya wizara yake bungeni jana, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema kuwa baadhi ya wabunge ambao wanashiriki kwenye vikao vya uamuzi vya TANESCO kama wajumbe, wamekuwa wakilihujumu shirika hilo kwa njia mbalimbali ikiwamo kufanya nalo biashara, "Shirika liliwahi kulipa Pauni za Uingereza 50,000 kwa ajili ya kununua vipuri, lakini kilicholetwa nchini ni masanduku ya misumari,” alisema Profesa Muhongo na kuongeza; “Hata katika nguzo za umeme kuna biashara inaendelea. Tunajua kuwa nguzo hizo zinazalishwa Iringa na kupelekwa Mombasa kisha kurudishwa nchini kwa maelezo kwamba zimetoka Afrika Kusini."

Waziri Muhongo alisema kuwa mbali na ufisadi huo, baadhi ya wabunge ambao ni wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini wamewahi kuliuzia shirika hilo matairi ya magari kwa bei kubwa, bidhaa ambayo hata hivyo alisema haina ubora unaokubalika,  "Baadhi ya wabunge wanafanya biashara na TANESCO; niseme tu kuwa, hii siyo sahihi. Lakini niombe kwamba mjadala huu tuufunge kwa sababu, tayari tumekabidhi suala hilo kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)" alisema Waziri Muhongo.

Waziri Muhongo pia alizungumzia jinsi baadhi ya watu na kampuni zinavyoiibia TANESCO kupitia mita za Luku ambapo aliwataja  watu hao kuwa ni pamoja na Shule za St. Mary's zinazodaiwa Sh10.5 milioni, Access Bank, Tawi la Tabata Matumbi Sh13.8 milioni na Hoteli ya Akudo Paradaise ya Kariakoo inayodaiwa Sh25.5 milioni.

Alisema kuwa baada ya kubainika kwa wadaiwa hao hutumia umeme kinyume na utaratibu,wahusika  wote walikamatwa na kufikishwa kituo cha polisi baada ya kufanyika kwa uchunguzi, “Baada ya kufanya uchunguzi na kubaini kuwapo kwa watu wanaotumia umeme bila kulipia na kuisababishia TANESCO hasara, tumeamua kuwachukulia hatua ikiwamo kuwafikisha polisi,” alisema Profesa Muhongo na kuongeza: “Inaonyesha wazi kwamba wizi wa umeme wa Luku umekuwa ukifanyika mara kwa mara na kwamba baada ya kuwakamata hawa, uchunguzi utaendelea na wengine watakaobainika watachukuliwa hatua za kisheria.”

Jenista Mhagama

Katibu wa Wabunge wa CCM, Jenista Mhagama alisema kuwa, amepokea kwa masikitiko taarifa hizo za wabunge wa CCM kuingia katika tuhuma hizo, lakini akasema namna nzuri ya kushughulikia tatizo hilo ni vyombo vya dola kufanya uchunguzi makini ili kujiridhisha na kisha hatua za kisheria kufuatwa, "Ni taarifa mbaya kwa kweli, lakini mimi niiombe Serikali itusaidie kufanya uchunguzi ili ukweli ubainike na hatua zichukuliwe," alisema Mhagama.

David Silinde

Naye Katibu wa Wabunge wa CHADEMA, David Silinde alisema: "Kwa kuwa tumesikia, kama kambi tutafanya uchunguzi juu ya tuhuma hizo. Tutakaa kikao cha kuamua nini cha kufanya. Pia tutatoa tamko juu ya mwenendo mzima wa hizi tuhuma na Bunge kwa ujumla.”

Zitto Kabwe

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Mashirika ya Umma ambayo imeunganishwa kwenye tuhuma hizo, Zitto Kabwe, alisema tuhuma hizo anazisikia, lakini anaziona kama siasa za majitaka kwa sababu zinarushwa bila ushahidi wowote, "Hakuna hata mbunge mmoja aliyesimama kusema nani amehongwa nini. Mimi binafsi sijahongwa na mtu yeyote wala mimi sijamtetea mtu isipokuwa natetea taratibu kufuatwa," alisema.

Zitto alibainisha kuwa anaamini tuhuma hizo zimetokana na hasira za yeye kupinga posho za wabunge na sasa wameona hilo ndilo eneo la kumkomoa, "Kwa kuwa ‘my conscious is clear’, (dhamira yangu safi) sina mashaka, uzushi, uongo na siasa za majitaka hizi zitaumbuliwa na ukweli. Hata hivyo, kwa kuwa tuhuma hizo zinasemwa juu juu tu, tutataka vyombo vya dola vichunguze na ikithibitika hatua zichukuliwe," alisema na kuongeza: "Kwangu mimi naona hizi ni siasa za urais na hasira za posho. Wenye kutaka urais wa vyama vyote na wapambe wao, wameungana kunichafulia heshima yangu. Wabunge wenye njaa ya posho, wameungana kunikomoa. Ukweli una tabia ya kutopenda kupuuzwa. Mwalimu Nyerere (Julius) alisema katika andiko lake la 'Tujisahihishe'.”

Mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) alishauri pia Spika wa Bunge kutumia Kamati ya Maadili kuchunguza tuhuma hizo kwa kuwa hazipaswi kuachwa zikapita hivihivi.

John Cheyo

Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali, John Cheyo alisema anasikitika kuona Bunge ambalo kimsingi ni kitovu cha uadilifu limeanza kuvamiwa na mafisadi, "Very unfortunate, (bahati mbaya sana) Bunge ambalo ni kilele cha uadilifu, nyumba ya waheshimiwa, ambako kunatarajiwa high level of intergrity (uadilifu wa hali ya juu), kuanza kutumika kama perpets (vibaraka) wa mafisadi," alisema na kuongeza: "Ninalaani sana kitendo hicho, lakini niwaambie viongozi wapya wa Wizara ya Nishati na Madini kuwa, waendelee kufanya kazi kwa uadilifu na nguvu yao ni wabunge wengi wema, ambao watawaunga mkono. Wasikate tama," alisema.

Mjadala ya wabunge

John Shibuda

Mbunge wa Maswa Magharibi (CHADEMA), John Shibuda aliliomba Bunge kufanya uchunguzi ili kuwabaini wabunge wanaojihusisha na vitendo vya rushwa.

Alisema tabia ya wabunge kuendelea kusema kwa mafumbo kwamba wapo baadhi ya wabunge wanatuhumiwa kwa rushwa, haina maana yoyote badala yake wahalifu hao wanatakiwa watajwe hadharani.

“Mheshimiwa Spika kumekuwa na maneno hapa kwamba wapo wenzetu wanakwenda kinyume na maadili yetu.

“Hao wanaosutwa ni bora watajwe ili wafahamike kuliko kunyamaza na kuendelea kushutumiana kwa porojo, kwa vionjo. Bila kuwataja watu hao tutakuwa tunalaumiana bure.

“Wabunge najisi watambuliwe. Hawa lazima watajwe kwa sababu sasa Bunge limekuwa kama bucha ya kuchinja watu, hatuwezi kukubali.

“Hivi kuna kitu gani kilicho kama sumaku kinachowavuta wabunge mpaka waanze kushutumiwa. Mheshimiwa Spika chunguza kwa makini uone ni sababu gani zinazosababisha wabunge waanze kutuhumiwa katika mambo dhalimu,” alisema Shibuda.

Aliwataka Waziri Profesa Muhongo na Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini, Eliachim Maswi, wawe makini na ikibidi wawachukulie hatua wafanyakazi wasiokuwa waadilifu.

“Katibu na Waziri mmerithi makosa yasiyokuwa yenu, waondoeni wabovu kwa sababu kama wakijiimarisha watakuwa kama vichuguu na mwishowe watajiimarisha na kuwaharibia.

“Waondoeni makunguru maana kunguru hafugiki hata ukimpa ubwabwa bado hafugiki. Mheshimiwa Spika tembo hubeba viroboto na kamwe viroboto hawabebi tembo. Je, tayari mmeshawapiga risasi viroboto wote wasiofaa?

“Waondoeni wabovu, watu najisi waondolewe kabla hawajawaondolea udhu wenu, tafadhari waondoeni hao.

“Hata nyinyi CCM ongezeni uadilifu ili muonekane kama Serikali yenu imeokoka na hatimaye muondokane na tingatinga linaloweza kuharibu kazi yenu,” alisema. 

Josephat Kandege Mbunge wa Kalambo, Josephat Kandege (CCM) aliwashutumu wabunge wanaoshutumiwa kwa rushwa ingawa hakuwataja kwa majina, “Mheshimiwa Spika ni kama siku sita hivi wabunge wamekuwa wakijadili mambo ya baadhi ya wabunge wenzetu. Watu hao wamekuwa wakisema hawataki posho, kumbe wana posho zao nzito nzito ambazo walikuwa wanazitaka. Wakati wanakataa posho, sisi tulikuwa hatuhangaiki kwa sababu tunataka hizi posho ndogo. Watu hao wamekuwa wakijipambanua kwamba ni waaadilifu lakini Mungu akitaka kukuumbua utaumbuka tu na nyinyi ni mashahidi. Nadhani Mheshimiwa Spika ujumbe wangu umefika na kwa uzito niliotarajia,” alisema Kandege na kuhamia katika mada nyingine.

Ally Keissy Mohamed
Ally Keissy Mohamed alisema kuna haja wahalifu hao wakatajwa kwa majina kwa kuwa hivi karibuni Profesa Muhongo na Maswi, walitumiwa ujumbe wa vitisho kutokana na uwajibikaji wao.

Kwa mujibu wa Keissy, kama wabunge hao hawatatajwa, viongozi hao wawili hawatakuwa na moyo wa kufanya kazi kwa sababu baadhi ya wabunge walimfuata Maswi na kumuomba Sh. milioni 50.

(nukuu ya  gazeti la MTANZANIA)

Kangi Lgora

Naye Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugora alitaka Waziri wa Nishati na Madini awataje wabunge aliowatuhumu ili kuonyesha usawa hasa baada ya kuwataja kwa majina watuhumiwa wengine katika ufisadi wa TANESCO na wale wanaoliibia umeme shirika hilo la umma, "Tunaomba waziri asema kwa nini asiwataje hao wengine wakati tayari ametutajia kina Freddy na Veronica William Mhando na taasisi za St Mary? " alihoji.

Hoja hiyo ya Lugora ilitupwa na Spika wa Bunge Anne Makinda aliyesema kuwa jambo hilo lina taratibu zake.

Vicky Kamata

Vicky Kimata (Viti Maalumu) nusura amwage machozi bungeni juzi jioni, alipozungumza kwa uchungu kupinga hatua ya wabunge hao kujihusisha na ufisadi, huku akieleza kuwa nchi imefika pabaya, 'Watanzania tumefikia hapo! Watu wanatengeneza mgawo wa umeme ili kujipatia hela, Jamani...jamani.. Hammwogopi hata Mungu!"

Said Mussa Zuberi alipendekeza itungwe sheria ya kuwanyonga mafisadi na wahujumu uchumi kwa kuwa matendo hayo pia ni uuaji, "Katika taifa letu tuna wadudu sijui tuwaite mchwa ambao wanaharibu yaliyotengenezwa kwa maslahi yao. Nawashauri wananchi kwa kuwa sasa tuko kwenye suala la Katiba, wasisahau kupitisha sheria ili watu wahujumu uchumi tuwaue, tena kwa risasi.

Vita kubwa TANESCO

Kuna kila dalili kuwa imeibuka vita ya wazi kati ya Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), huku Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO aliyesimamishwa kazi, William Mhando, akipigiwa debe la wazi na wabunge.


Taarifa zilizopatikana kwenye ofisi za Bunge zinasema kuwa Kamati ya Nishati na Madini inajipanga kukwamisha bajeti ya wizara hiyo kama Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO aliyesimamishwa kazi, Injinia Mhando, hatarejeshwa kazini huku wizara ikisisitiza kuwa amesimamishwa kazi kupisha uchunguzi wala hajafukuzwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Zitto Kabwe, naye ana msimamo kuwa Mhando ameonewa na wizara inaweza kujiokoa kwa kumrejesha ofisini kisha ufanywe uchunguzi maalumu utakaoendeshwa na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG).

“Unajua kilichopo ni mvutano baina ya Kamati (ya Bunge) na Katibu Mkuu (Maswi). Yeye anasema alikiuka Sheria ya Ununuzi wa Umma kwa sababu ya uzalendo. Anasema mimi Munde na Sara Msafiri tunafanya biashara ya matairi na TANESCO, ndiyo maana tunaipigia debe TANESCO.

Aliwaambia waandishi wa habari kuwa tangu alipoteuliwa aliwaambia wazi watumishi wa wizara hiyo kuwa anataka kurejesha heshima ya Serikali ndani ya Wizara ya Nishati na Madini, anataka kuondoa ubadhirifu na la mwisho ni kuwa na uwazi katika kazi zinazofanywa na wizara.

“Nimewaambia wazi kuwa asiyeyaweza hayo afunge mizigo aondoke,” alisema Maswi.

Mhando adaiwa kuomba msaada wa Simbachawene

Awali, Katibu Mkuu aliiambia JAMHURI kuwa Mhando alikuwa amepita kwa Naibu Waziri Simbachawene akimtaka amsaidie kumlinda, kwa maelezo kuwa Katibu Mkuu hampendi yeye (Mhando).

“Mhando alikwenda kwa Naibu Waziri Simbachawene akamwambia anaomba amlinde kwani mimi simpendi. Simbachawene akamwambia Waziri Muhongo, Waziri akamwambia Simbachawene mwambie Katibu Mkuu, akaniambia.

“Mimi nikamwita. Nikamwambia unasema sikupendi kivipi? Nikamwambia mimi Kama Maswi na wewe kama Mhando tunaweza kuwa marafiki lakini urafiki wetu si wa MD au Katibu Mkuu. Hivi ni vitu viwili tofauti. Nilimwita nikamuuliza mimi nikupende wewe unataka uwe mchumba wangu?

“Tangu mwanzo niliwaambia wakurugenzi wote msijipendekeze kwangu. Mtu anayetaka kuja kwangu afanye kazi. Mhando akawa hafanyi kazi, anazunguka anatafuta jinsi ya sisi kukubaliana naye tumsaidie. Anatuma watu nimsaidie kufanya kazi, nimsaidie nini? Kufanya kazi ipi?

“Siku moja nikamwita nikamwambia nikusaidie nini? Mimi nafikiri hunielewi. Nikamwambia wewe ni rafiki yangu kama Mhando na Maswi, lakini kama MD na Katibu Mkuu ni vitu viwili tofauti,” alisema Maswi.

Mhando atuhumiwa kumpa kazi mkewe

Tuhuma nyingine anazochunguzwa nazo Mhado kwa sasa ni kwamba alimpatia mke wake zabuni ya kuuza stationery kupitia kampuni ya Santa Clara. Kampuni hii imepewa mkataba wa Sh milioni 800 kuiuzia TANESCO.

Mke wa Mhando sasa anafahamika kama Eva Stephen William wakati zamani alifahamika kama Eva Stephen Mhando.

Mikataba 23 inachunguzwa, lakini pia mitatu inayofanyiwa kazi mara moja ni ununuzi wa mita za Luku kwa bei mara mbili ya bei halisi, mkataba wa ku-supply  stationery na ununuzi wa vifaa vyenye ubora usioridhisha.

Mboma adaiwa kumpigia debe Mhando

Wiki ya Juni 17, Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Jenerali mstaafu Robert Mboma, anadaiwa alikwenda Dodoma na Mhando wakiwa kwenye gari moja kufanya uzengezi kuhakikisha Mhando anarejeshwa madarakani, lakini inadaiwa aligonga mwam ba. Juhudi za kumpata Jenerali Mboma zimegonga mwamba kwani simu yake inaita bila kupokewa.

Maswi ahoji nia ya wabunge

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Maswi alihoji inakuwaje wabunge wanamtetea kwa kiwango kikubwa Mhando aliyesimamishwa kazi kwa utaratibu sawa na ilivyotokea kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Charles Ekelege, lakini hakuna anayependekeza Ekelege aendelee kuwa kazini wakati uchunguzi ukiendelea?

“Alikuja kwenye Kamati tarehe 17 Juni may be (labda) akidhani amepata kitu kinaschotaka kugawa wajumbe. Kama wajumbe, mimi nikawaambia wajumbe hawa ikithibitika nafanya biashara na TANESCO niko tayari kujiuzulu hadi ubunge. Hata hivyo, si kosa kufanya biashara isipokuwa unapaswa ku-declare interests (kutangaza mgongano wa kimasilahi).

“Zedi akamwambia ulitaja majina ya wabunge wanaofanya biashara na TANESCO yeye akasema sikutaja. Mwenyekiti akamwambia Katibu Mkuu ‘nadhani una matatizo’. Sara akasema hafanyi biashara yoyote na TANESCO na akamtaka atoe vithibitisho… Katibu Mkuu akasisitiza kuwa hajawataja hao wabunge,” alisema Tambwe.

Mbunge huyo alisema Serikali inawachanganya, kwani wakati wizara inadai TANESCO wanaiba bilioni 60 kila mwezi, CAG amelipatia shirika hilo hati safi.

“[Christopher ole] Sendeka akamwambia tatizo lako Maswi unataka ubabe na Sara [Msafiri] akamwambia Katibu ukiwa mchawi utakula watoto wa jirani unamaliza, kisha utakwenda kula wa kwako,” alisema Tambwe akiwakariri wabunge hao wakimsihi Maswi aachane na mpango wa kumsimamisha kazi Injinia Mhando.

Alisema bajeti ya mwaka jana iligomewa Serikali ikasema itawapa hela ya mpango wa dharura Sh bilioni 408, lakini hadi leo TANESCO wananunua umeme bei kubwa kisha wanauza kwa bei ndogo. “Nasema suluhisho ni kununua mitambo ikamilikiwa na TANESCO si kuendelea na utaratibu huu wa kukodisha,” alisema.

Hata hivyo, Tambwe alisema vita yote iliyopo ni kwamba wizara na TANESCO wanagombea kununua mafuta kwani huko ndiko kwenye ulaji.

Msafiri amsema Maswi

Mbunge wa Viti Maalum ,Sara Msafiri (CCM), alipoulizwa tuhuma dhidi yake alisema: “Hizo ni mbinu chafu zinazofanywa na Katibu Mkuu Maswi na Waziri wake kuwatisha, kuwaziba midomo na kuwagawa wabunge hasa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini.

Kwenye kikao Katibu Mkuu wa Wizara alitakiwa kuthibitisha tuhuma hizo, walisema wanayo orodha ya majina ya wabunge wanaofanya biashara, lakini ndani ya Kamati ya Nishati na Madini hakuna yeyote anayefanya biashara na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati na Madini.

“Aidha, si dhambi kwa Mbunge kufanya biashara, anachotakiwa ni kutangaza ili kuepuka mgongano wa kimasilahi.”

Zitto aitahadharisha Wizara, Waziri Mkuu

Kwa upende wake, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Zitto Kabwe, anasema anachopinga ni unyanyasaji dhidi ya watumishi wa umma na si vinginevyo.

“Sijatangulizwa na mtu kumtetea Mhando, kwani ni wajibu wangu kama Mwenyekiti wa Bunge wa Kamati ya Mashirika ya Umma kuhakikisha kwamba mashirika yanaendeshwa kwa mujibu wa sheria na kanuni.

“Philosophia ya ‘eyes on hands off’ ndiyo inayotakiwa itumike. Sitaki micro-management (wizara kuingilia). Na hii si mara ya kwanza. Consolidated Holding nilimwonya [Mustafa] Mkulo kuingilia mashirika alipomsimamisha [Methusela] Mbajo nilihakikisha anarejeshwa kazini.

“Mimi ni muhanga wa kuonewa. Mtu ambaye hajaonewa ndiye anayeweza asimtetee mtu anayeonewa. Katika suala la TANESCO, Waziri na Katibu Mkuu wako wrong (wamekosea).

“Sina masilahi TANESCO, sina biashara TANESCO, sijahongwa, naongea kwa uzoefu. Hata Dk. Rashid wakati anashambuliwa nilisimama kumtetea kwa sababu naamini katika ukweli.

Nimeiambia Kamati kwenye TANESCO ‘they are wrong’ (wamekosea). Waziri Mkuu [Mizengo Pinda] nimemwambia action ya TANESCO is wrong. Inawezekana TANESCO kuna uchafu lakini hatua hazichukuliwi kwa njia hii.

“Nikiwaacha Maswi na Muhongo kufanya haya bila kuhojiwa, itawazuia nini mawaziri wengine kufanya walichokifanya? Nimezungumza nao wote - Waziri Mkuu, Maswi, Muhongo, [George] Simbachawene - nikawaambia mrejesheni ofisini Mhando.

“Kagasheki aliposimamisha watu waliosababisha faru kuuawa, sikusema kwani alifuata utaratibu. [Dk. Harrison] Mwakyembe alipomsimamisha Mkurugenzi Mkuu wa ATC nilimuonya Mwakyembe kuwa ‘you are wrong’ (umekosea), bahati yule Mkurugenzi Mkuu wa ATC alikuwa hajathibitishwa kazini ndiyo ikamuokoa.

“Nilimzuia Mwakyembe kumsimamisha Mkuu wa Chuo cha Mabaharia (DMI), nikamwambia ukim-touch (ukimgusa) tutakumaliza. Inawezekana kabisa wanatetea haki lakini kuna taratibu za kufuata.

“TANESCO walitoa tenda na BP wakabid, Camel Oil wakabid, lakini BP wakabid bei kubwa kuliko wote hawa. Walibidi Sh 1,900 kwa lita wakati wengine walibid Sh 1,800. Baadaye kwa mlango wa nyuma wakaenda ku-negotiate kuuza kwa bei ndogo. Kwa nini waliposhindwa tenda wakaenda mlango wa nyuma kuuza kwa bei ndogo?

“Tunafurahi kwamba tumepata mafuta kwa bei ndogo, lakini Wizara ‘is a different procurement entity’ (taasisi tofauti ya ununuzi), hata kama unafanya hayo manunuzi, kwa nini kwanza usingekwenda kuwafuata hao Oryx na Camel Oil ukasema tupunguzie wakakataa ndipo ukachukua hatua hiyo?

“Katibu Mkuu si ‘procurement authority’ (si mamlaka ya ununuzi). Kwa nini yalitumika mazungumzo kati ya Katibu Mkuu na kampuni? Kwa nini hukuandika barua PPRA kuomba wakushauri? Nikamwambia hii ingekulinda.

“Nimehoji matukio mawili yanatofauti gani? Edward Lowassa ameng’olewa Uwaziri Mkuu si kwa sababu amepewa hela, kwa sababu Richmond haikupewa hata senti tano bali sheria ya manunuzi haikufuatwa. Hilo tu ndilo lililomgharimu Lowassa… kwa nini leo tusema sheria ya manunuzi haiwahusu hawa? Kwa sababu si Lowassa au Rostam [Aziz]?

“Baadhi ya wabunge wanataka Maswi na Muhongo waondoke, mimi nasema hapana.

Isije ikawa kwa sababu tuna ubavu tuwatimue tu, ninachosema Mhando arudishwe kazini. CAG atafanya ukaguzi ukweli ujulikane. Mimi nimekwenda kufanya ukaguzi miezi miwili iliyopita nimekuta PPRA imetoa clean certificate kwa TANESCO. Kama tunahisi kuna uchafu ambao hawakuuona tufuate taratibu,” alisema Zitto.

Suala la wabunge kufanya biashara na TANESCO, alisema hata yeye amezisikia tuhuma hizo kuwa wabunge hao wanatumiwa na mfanyabiashara mwenye asili ya Kiasia (jina limehifadhiwa), kuuza matairi na bidhaa nyingine kwa TANESCO lakini hana uthibitisho wa taarifa hizo.

Alimshangaa Waziri Muhongo kwa kusema TANESCO inakusanya Sh bilioni hadi 70 na inatumia bilioni 11 tu kulipa mishahara, hivyo akataka fedha zinazobaki wazitumie kulipa madeni.

“Asilimia 86 ya mapato ya TANESCO yanalipa makampuni yanayozalisha umeme - Songas, IPTL, Symbion na mengine. Na hii mikataba imeingiwa na Serikali. Kwa mfano, Symbion sasa wana mkataba wa miaka 20. Mimi nilimwambia Katibu Mkuu kuwa mnawapa Symbion zabuni ya kuzalisha umeme megawati 300 huko Mtwara, hivi Marekani ikiamua kuiteka nchi hii tutatokea wapi?

Zito aliwataka viongozi wa Wizara ya Nishati na Madini na TANESCO kuacha vita ya kupitia kwenye vyombo vya habari, Mhando arejeshwe kazini na CAG afanye ukaguzi maalumu kwenye shirika hilo.

“Sitaki Maswi aonewe, wala sitaki yeyote aonewe. Ninaumizwa mno na vurugu zinazoendelea kati ya wizara na TANESCO. Hii ni vita ya masilahi waachane nayo. Tunataka umeme hatutaki maneno,” alisema Zitto.

Zitto alikemea alichokiita utamaduni wa kuwaona watu wenye maoni fulani na waliyonayo baadhi ya watu kuwa wamehongwa. “Ni utamaduni wa hovyo sana.”

Zitto alisema inawezekana Katibu Mkuu Maswi amefanya uamuzi wa kununua mafuta kutoka BP/Puma kwa nia njema, kisha akamnukuu Mwalimu Julius Nyerere: “Njia ya kwenda Jehanamu imejaa nia njema’.”

Maswi aanika ukweli wa mambo

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Maswi, kwa upande wake jana alikutana na waandishi wa habari na kusema wabunge wajiepushe na upotoshaji usio wa lazima, kwani Wizara ya Nishati na Madini haikufanya ununuzi wa mafuta, badala yake wizara hiyo ililipa tu na kazi ilifanywa na Wakala wa Vizazi na Vifo (RITA) ambaye kwa amri ya mahakama ndiye mfilisi wa IPTL.

“Ni vizuri ikaeleweka kuwa mwishoni mwa mwaka 2010/11 kulikuwa na mgawo mkubwa wa umeme nchini, hivyo Serikali kulazimika kuingilia kati kuhakikisha mgawo huo unaondolewa na kuitaka IPTL kuwasha mitambo yake katika kiwango cha MW 100. Aliyefanya hivyo ni Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO na si Wizara.

“Ikumbukwe pia wakati IPTL ilipokuwa inasimamiwa na RITA kwa kuwa kulikuwa na amri ya kuifilisi (under liquidation)… TANESCO walipeleka barua RITA wakitaka mafuta ya kuendesha mitambo yapatikane. Ieleweke kuwa ili kuendesha mitambo ya IPTL kwa siku moja tunahitaji MT 500.

“Tarehe 24 Juni 2011, Mtendaji Mkuu wa RITA aliandika barua PPRA yenye Kumb. Na. BD.27/249/01/19 kutoka mwongozo na ushauri juu ya ununuzi wa mafuta ya kuendesha mitambo ya IPTL kwa dharura na barua hiyo ikajibiwa na Mtendaji Mkuu wa PPRA, tarehe 28 Juni, 2011 kwa kumpa njia na mwongozo wa kutumia wakati wa dharura kwa kufuata Sheria ya Manunuzi na bila kukiuka utaratibu.

“Mtendaji Mkuu wa RITA kwa barua yake yenye Kumb. Na. ADG/OR/1/2008/IPT/VOL. II/47A ya Julai 2011 na kupokelewa wizarani siku hiyo hiyo, alionyesha mchakato wa manunuzi uliofanyika na taratibu zinavyotakiwa.

“Baada ya kupokea barua hiyo na kutokana na hali ilivyokuwa, hakuna aliyekuwa tayari kuhangaika na IPTL wala mafuta hadi nilipoteuliwa kuja kukaimu hapa tarehe 22 Julai 2011 na kuanza kazi tarehe 25 Julai 2011. Fedha zinazosemwa zililetwa wizarani ni za Serikali na si za TANESCO, Afisa Mwajibikaji (Accounting Officer) ni wa Wizara si TANESCO,” alisema Maswi.

Alisema Kanuni ya Ununuzi wa Umma Na. 42 ya Mwaka 2005 inampa mamlaka afisa anayewajibika na fedha kufanya manunuzi hata nje ya mipaka yake kwa masilahi ya uchumi wa taifa.

“Napenda ifahamike wazi kuwa hapa kilichofanyika ni kuwa RITA ndiye aliyefanya ununuzi, sisi wizara tulifanya kazi ya kulipa tu,” alisema na kuongeza kuwa fedha zilizotumiwa ni za Serikali na hazikutoka TANESCO kama inavyoelezwa.

Alisema suala jingine ni kwamba wakati kampuni zilizopewa zabuni awali kuuza mafuta TANESCO zilikuwa zinauza kwa gharama ya Sh 1,800 kwa lita, BP/Puma wanauza lita hiyo hiyo kwa Sh 1,460. Pia BP ni mbia wa Serikali kwa asilimia 50 kwa 50 tofauti na kampuni zinazong’ang’aniwa ambazo ni binafsi. “Kuokoa Sh bilioni 2.7 za walipa kodi si fedha kidogo,” alisisitiza.

Alisema kampuni zilizokuwa na zabuni ya kuuza mafuta TANESCO zilikuwa zikinunua mafuta kutoka BP, walionyimwa zabuni ya kuuza mafuta kisha zinaiuzia TANESCO, kitu alichosema kinahitaji kuchunguzwa kwa nini iwe hivyo.

Mkopo wa Sh bilioni 408 kwa TANESCO

Maswi alisema mkopo huo una riba kubwa na utalipwa na wananchi, hivyo Serikali imeamua kwa njia nyingine wakati taratibu za kufuatilia mkopo zikiendelea, yenyewe imekuwa ikitoa ruzuku kwa TANESCO na hadi sasa imekwishatoa zaidi ya Sh bilioni 222.4. Alisema hadi juzi Serikali imetoa ruzuku ya Sh bilioni 25 kwa TANESCO, hivyo watu wasiibe wimbo wa bilioni 408 ambazo ni gharama kubwa kwa walipakodi.

Maswi asisitiza mambo makuu matatu

Kama ilivyokuwa mwaka jana, siku chache kuelekea kwenye bajeti ya wizara hiyo ilipokataliwa, kuna kila dalili kuwa zamu hii suluba bado itakuwa kubwa kwa viongozi wakuu wa wizara hii; Waziri Profesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wake, Eliakimu Maswi, kwani wabunge wameshaanza kurusha mashambulizi.

Kikao cha Kamati ya Bunge Julai 17

Katika kikao cha Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini cha Julai 17 kilichofanyika mjini Dodoma, imeelezwa kuwa kilijaa vijembe, maneno mazito na kutunishiana misuli kati ya wabunge na uongozi wa Wizara ya Nishati na Madini.

Huku Kamati hiyo ikiwa na msimamo kuwa Prof. Muhongo na Katibu Mkuu Maswi wajiuzulu kwa wanachokiita kashfa ya kuipatia Kampuni ya Puma zabuni ya kuuza mafuta kwenye mitambo ya IPTL bila kufuata taratibu za ununuzi wa umma, wizarani nako kuna hisia kuwa baadhi ya wabunge wanajifanya kuitetea TANESCO, kumbe wanatetea masilahi binafsi yanayobanwa na uongozi mpya wa wizara usiokuwa tayari kuyumbishwa.

Mbunge wa Viti Maalum, Munde Tambwe (CCM), aliliambia Gazeti la JAMHURI kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Maswi, alimpigia simu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Seleiman Zedi, na kumwambia baadhi ya wabunge wanafanya biashara na TANESCO ndiyo maana wanashinikiza Injinia Mhando arejeshwe kazini.


Deodatus Balile,
JamhuriMedia.co.tz

Usalama wa Taifa wapinga kumdhuru Dk Stephen Ulimboka


Dk Stephen Ulimboka akiwa chumba cha wagonjwa mahututi Muhimbili
IDARA ya Usalama wa Taifa wa Tanzania imepinga kuhusika kwenye tuhuma zinazotolewa na baadhi ya vyombo vya habari kuwa inahusika na sakata la kutekwa, kuteshwa na hatimaye kujeruhiwa vibaya kabla ya kutupwa msituni kwa kiongozi wa madaktari nchini Stephen Ulimboka
Kwa mujibu wa taarifa yake kwa vyombo vya habari idara hiyo imesema; “katika siku za hivi karibuni, kumejitokeza taarifa zenye tuhuma kadhaa dhidi ya Idara ya Usalama wa Taifa. Taarifa hizo zimekuwa zikitolewa kwenye vyombo vya habari zikiihusisha Idara hii na matukio ambayo yanaidhalilisha na kuzua maswali mengi kwa wananchi.”
“Kati ya tuhuma hizo ni tukio la kutekwa kwa Dk. STEPHEN ULIMBOKA, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari na madai ya kufanywa kwa mipango ya kuwadhuru baadhi ya Viongozi wa Vyama vya Upinzani. Gazeti moja la kila wiki limekuwa likurudia tuhuma hizo mara kwa mara kwa madai kwamba ni habari za uchunguzi na kuihusisha Idara”.
Taarifa hiyo imesema taarifa zinazotolewa dhidi yake ni UZUSHI na UONGO ambazo zina nia ya kuharibu jina na sifa ya Idara. Taarifa hizo zimekuwa zikiunganishaunganisha vipande vya taarifa mbalimbali ili kukidhi malengo yaliyokusudiwa na wanaolitumia gazeti hilo. Idara haikuhusika wala haihusiki na matukio yoyote yaliyotajwa katika tuhuma hizo.
“Hivyo tunawaomba wananchi wazipuuze taarifa hizo. Matukio yaliyotajwa katika tuhuma hizo yanachunguzwa na Jeshi la Polisi ambacho ndicho Chombo Chenye Dhamana, na kwa Maslahi ya Taifa si vizuri kuachia upotoshaji huo uendelee.”
“…tunapenda kuwahakikishia Watanzania kuwa uzushi na tuhuma zinazotolewa dhidi ya Idara hazitatuvunja moyo bali zitatuunganisha na hivyo kutuimarisha katika azma yetu ya kuhakikisha nchi yetu inaendelea kubaki salama kwa kushirikiana na wanachi na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama.” Ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Short URL: http://www.thehabari.com

Friday, July 27, 2012

Zitto-Nisihusishwe na Matamshi na Makanusho ya Wabunge walokuwa Kigoma




Na Zitto Kabwe
KATIKA gazeti la Mwananchi la tarehe 23 Julai 2012, kulikuwa na habari yenye kusomeka ‘Wabunge wamsafishia Zitto njia ya Urais 2015′. Habari hii imeleta mjadala mara baada ya kutoka na kusomwa. Mjadala umekuzwa zaidi baada ya Wabunge ndugu Halima Mdee na ndugu Joshua Nassari kukanusha maneno waliyonukuliwa kuyasema. Napenda kusema masuala yafuatayo.
Moja, Waheshimiwa Wabunge Halima Mdee, Joshua Nassari, Kangi Lugola, Esther Bulaya, Deo Filikunjombe, Raya Ibrahim, Amina Mwidau na David Kafulila walihudhuria tamasha la vijana wa Kigoma All Stars kwa kualikwa na Mratibu wa kundi hilo Mwasiti Almasi.
Wabunge wengine walialikwa lakini hawakutokea wakiwemo Joseph Mbilinyi, David Silinde, Amos Makala, Vicky Kamata na Peter Serukamba. Wabunge hawa hawakualikwa na mimi bali nilisaidia ‘logistics’ tu. Lengo la kushauriana na Vijana wa Kigoma All Stars kuwaalika wabunge kutoka vyama mbalimbali lilikuwa ni kuonyesha umoja na mshikamano wa nchi bila kujali vyama vya siasa.
Wabunge wote walioalikwa waliambiwa hii ni shughuli ya muziki na wala sikufanya mazungumzo nao yeyote ya awali au kuwaambia au kukubaliana nini cha kuzungumza au hapana. Tamasha lilikuwa la muziki na halikuhusika kabisa na siasa. Ni bahati mbaya sana kuwa kuna matamshi ya kisiasa yalitamkwa katika shughuli ile.
Waheshimiwa wote walipewa nafasi ya kusalimia na wote walizungumza. Wabunge waliozungumza kwa muda mrefu kidogo ni ndugu Halima Mdee, Joshua Nassari, Deo Filikunjombe na Kangi Lugola.
Hotuba za Wabunge wote zilirekodiwa kwenye video neno kwa neno na video hizo zitawekwa wazi kwenye blogu yangu kama sehemu ya documentary ya tamasha lile la kihistoria.
Pili, sikuhusika kwa namna yeyote ile na kuandikwa kwa habari hii iliyozusha mjadala. Wala sikujua kama habari hii ingeandikwa maana katika ziara ile sikuita mwandishi hata mmoja maana nilitaka liwe tukio la Kigoma tu. Mimi kama mlezi wa KigomaAllStars na vijana wenyewe tulijikita katika ‘shukrani Kigoma’ kwa watu wa Kigoma.
Kama mwandishi kaandika ambayo wabunge hawa hawakuyasema basi itaonekana kwenye videos hizo. Wabunge wenyewe wanajua kwenye nafsi zao nini walisema Kigoma na kipi kiliwasukuma kusema walioyasema Kigoma.
Nisingependa kuhusishwa kwa njia yeyote ile na matamshi yao, habari iliyowanukuu na hata makanusho yao. Maana mwisho wa siku ukweli ndio utasimama.
Suala la Urais lisitupotezee muda kwani kuna mambo mengi sana ya kujadili kuhusu nchi yetu. Taharuki ambazo watu wanazipata masuala ya urais yanapotajwa zinashangaza sana. Chama changu bado hakijatangaza rasmi mchakato wa kupata mgombea Urais. Hivi sasa chama hakina mgombea Urais mpaka hapo mchakato utakapotangazwa ambapo wanachama wataruhusiwa kuomba kupeperusha bendera ya chama. Mwanachama wa chama chetu atakaye kubalika na jamii na wajumbe wa mkutano wa uteuzi ndiye atakuwa mgombea wetu. Kwa sasa hayupo na hivyo tusipoteze muda kujadili jambo hili.
Mzee Thabiti Kombo alituachia usia tunapokuwa tunazungumza. Alisema ‘weka akiba’ sio akiba ya fedha, bali ya akiba ya maneno. Tuweke akiba ya maneno. Tusimalize yote.

Wednesday, July 25, 2012

Farijara Hussein; Rajabu Maranda wamehukumiwa kufungo cha miaka 3

KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rajabu Maranda na ndugu yake, Farijala Hussein, wamehukumiwa kifungo cha miaka 18 jela, baada ya kukutwa na hatia katika makosa sita, yakiwemo ya kujipatia Sh bilioni 2.2 kutoka katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), iliyopo Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Washitakiwa wamehukumiwa kifungo cha miaka mitatu kwa kila kosa kwa makosa sita, lakini adhabu hiyo inakwenda kwa pamoja kwa hivyo watatumikia miaka 3 tu.

Washitakiwa hao, walitiwa hatiani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na jopo la mahakimu watatu, Projest Kahyoza, Fatuma Masengi na Catherine Revocath.

Mahakimu hao, walitofautiana katika uamuzi, hali iliyosababisha kuandaa hukumu mbili, moja iliandaliwa na mahakimu wawili, Kahyoza na Revocath na hukumu ya pili, iliandaliwa na Masengi.

Hukumu iliyoandikwa na mahakimu wawili ndiyo inayochukuliwa kuwa ya mahakama, ambayo imewatia hatiani washitakiwa hao na hukumu ya Masengi iliwaachia huru washitakiwa wote kwa madai upande wa mashitaka, ulishindwa kuthibitisha mashitaka bila kuacha shaka.

Akisoma hukumu ya kwanza, Kahyoza alisema washitakiwa walikuwa wanakabiliwa na makosa saba ya kula njama, kughushi, kutoa nyaraka za uongo, kughushi, kutoa tena nyaraka za uongo, wizi na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

“Katika mashitaka ya kughushi, hakuna shaka kwamba upande wa mashitaka waliweza kuthibitisha kosa, kwani waliokuwa wakidaiwa kuwa wamiliki halali wa Kampuni ya Money Planner & Consultant, hawajawahi kuwepo ni wa kufikirika.

“Washitakiwa walitumia majina hayo kwa udanganyifu, wakionyesha kwamba waliteuliwa kuiwakilisha Kampuni ya Kijerumani, B. Grancel kudai madeni BoT wakati si kweli,” alisema.

Alisema washitakiwa hakuna shaka kwamba walighushi hati iliyokuwa ikiwaruhusu kuchukua fedha za kampuni hiyo na kwamba taratibu zilifuatwa na waliwekewa kiasi cha fedha katika akaunti yao, iliyokuwepo Benki ya Biashara Afrika.

Alisema nyaraka za kuomba kulipwa kiasi hicho, zilikaguliwa na viongozi mbalimbali wa BoT na kuona zilikuwa sahihi bila kubaini zimesainiwa na upande mmoja wa Kampuni ya B. Grancel.

“Hati zilikuwa zimesainiwa na Jonath wa Kampuni Grancel ya Ujerumani, lakini Fundi Kitunga na Paul Thobias wa Kampuni ya Monney Planner hawakusaini.”

Upande wa mashitaka, umeweza kuthibitisha washitakiwa walitumia hati za kughushi kuchukua fedha BoT na shitaka la saba la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu limethibitika, kwani nyaraka za kughushi zilitumika na shtaka hilo lilishathibitika pia.

Pia upande wa mashitaka, uliweza kuthibitisha bila kuacha shaka kwamba, washitakiwa walikula njama na walishindwa kuthibitisha bila kuacha shaka katika shtaka la sita kwamba waliiba Sh 660,210,000.

Alisema wakiachia mbali shtaka la sita, washitakiwa wanatiwa hatiani katika mashtaka yote sita yaliyobaki kutokana na upande wa mashitaka kuthibitisha, bila kuacha shaka kwamba walitenda makosa hayo kwa nia mbaya.

Alisema hakuna ushahidi uliotolewa mahakamani na upande wa mashitaka ukionyesha kwamba Kampuni ya Kijerumani ya Gransel haikuwepo, haikuwa inaidai BoT na wala haikuwaruhusu Kampuni ya Money Planner kudai madeni yao.

Akisoma adhabu, Hakimu Revocath alisema washitakiwa wanahukumiwa kutumikia kifungo cha miaka mitatu katika kila kosa kwa makosa sita, lakini adhabu hiyo inakwenda kwa pamoja, “Washitakiwa watatumikia kifugo cha miaka mitatu mitatu kwa kila kosa, adhabu itakwenda kwa pamoja na inaanza leo (jana),”alisema Revocath na kuongeza adhabu hiyo kwa kosa la kwanza, pili, tatu, nne, tano na saba.

Sikukuu ya Mashujaa kufanyika Dar


Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wakitoa heshima kwenye mnara wa kumbukumbu ya Mashujaa katika viwanja vya mnazi mmoja leo ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya sherehe za maadhimisho ya kumbukumbu ya mashujaa.
Askari Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) watakaoshiriki kwenye gwaride wakati wa maadhimisho ya siku ya mashujaa wakiendelea na mazoezi katika viwanja vya mnazi mmoja jijini Dar es salaam.
Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Saidi Meck Sadiki (katikati) akiongea na waandishi wa habari Katika viwanja vya Mnazi mmoja leo jijini Dar es Salaam kueleza namna mkoa ulivyojipanga kufanikisha sherehe za maadhimisho ya siku ya mashujaa itakayofanyika kitaifa tarehe 25, Julai 2012 katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es salaam
Balozi Khalfan Juma Mpango kutoka Kongo

Monday, July 23, 2012

CCM ilivyoiteka Kigoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala wa Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI,) Aggrey Mwanri akihutubia, kwenye mkutano wa CCM uliofanyika, jana , Julai 22, 2012, kwenye Uwanja wa Community Centre, Mwanga mjini Kigoma.
Naibu Waziri wa Uchukuzi, Charles Tzeba akihutubia kwenye mkutano wa CCM uliofanyika, jana , Julai 22, 2012, kwenye Uwanja wa Community Centre, Mwanga mjini Kigoma.
Wazee kwenye mkutano wa CCM, Uwanjwa wa Community Cetre Mwanga Kigoma
Waziri wa Nchi Ofsi ya Rais, Mahusiano, Steven Wasira akihutubia kwenye mkutano wa CCM uliofanyika, jana , Julai 22, 2012, kwenye Uwanja wa Community Centre, Mwanga mjini Kigoma.

Waliokufa na Mv. SKAGIT Zanzibar waombewa

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein, (wa tano kushoto) pamja na Viongozi wengine wa Serikali wakiungana na Waislamu katika Swala ya kuwaombea Dua Abiria waliofariki katika Ajali ya Meli Mv Skagit ya Kampuni ya Seagul, iliyozama hivikaribuni ikitokea Dar es Salaam kuelekea Zanzibar, swala hiyo ikiongozwa na Mufti wa Zanzibar Sheikh
Saleh Omar Kabi, katika Msikiti wa Mwembeshauri Mjini Zanzibar leo. [Picha na Ramadhan Othman Ikulu.]
Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, leo ameungana na viongozi mbalimbali wa Kitaifa katika dua maalum ya hitma pamoja na Sala maalum ya Maiti (Salatul Mayyit al-ghaib), iliyosomwa huko katika msikiti Mushawar, Mwembeshauri mjini Zanzibar.
Sala na dua hiyo ni maalum kwa ajili ya kuwaombea watu waliokufa kutokana na ajali ya kuzama kwa meli ya MV SKAGIT, iliyotokea hivi karibuni wakati meli hiyo ilipokuwa inasafiri kutoka Dar es Salaam kuja Zanzibar na kusababisha vifo na majeruhi kadhaa
Katika sala na dua hiyo viongozi mbali mbali wa dini, vyama na Serikali walihudhuria akiwemo Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muunganao wa Tanzania Dk. Mohammed Kharib Bilal, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, Rais mstaafu wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume.
Viongozi wengine waliohudhuria ni Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Omar Khabh, Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji, Spika wa Baraza la Wawakishi Pandu Ameir Kificho, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharib Abdalla Mwinyi Khamis, Mawaziri, Manaibu Waziri, Wabunge, Wawakilishi, Mashekhe mbali mbali wa Zanzibar na Tanzania Bara pamoja na wananchi na viongozi wengine

Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano wa Zanzibar,Mh Hamad Masoud Hamad Ajiuzulu

.


Salma Said Mwandish wa Dw,

Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano wa Zanzibar, Hamad Masoud Hamad amejiuzulu wadhifa wake leo jioni imeelezwa. Kwa mujibu wa taarifa ya Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee ilisema tayari Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk. Ali Mohammed Shein amekubali ombi la Waziri Hamad Masoud kujiuzulu.
“Tarehe 20 Julai,2012 Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Mheshimiwa Hamad Masoud Hamad alimuandikia barua Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk Ali Mohammed Shein ya kumuomba ajiuzulu kufuatia ajali ya kuzama kwa meli ya Mv. Skagit iliyotokea Julai 18,2012” Ilisema taarifa ya Dk. Mzee.
Kufuatia kujiuzulu kwa waziri huyo, Rais Dk Shein amemteua Mwakilishi wa Jimbo la Ziwani(CUF) Rashid Seif Suleiman kuwa Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano.
“Kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano,Rais amemteua Rashid Seif Suleiman kuwa Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano” Taarifa ya Ikulu ilisema.
Uteuzi wa Waziri mpya wa Miundombinu na Mawasiliano umeanza Julai 23 mwaka huu.
Wakati huo huo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk. Ali Mohammed Shein ameunda Tume ya kuchunguza ajali ya kuzama kwa meli ya Mv. Skagit.
Mwenyekiti wa Tume hiyo ni Jaji Abdulhakim Ameir Issa, wajumbe ni Meja Jenerali S.S. Omar, COMDR. Hassan Mussa Mzee, Kapteni Abdulla Yussuf Jumbe, Kaptein Abdulla Juma Abdulla, Salum Taoufiq,Kaptein Hatibu Katandula, Bi. Mkali Fauster Ngowo, Ali Omar Chengo na Shaaban Ramadhan Abdalla Katibu wa Tume.

Saturday, July 21, 2012

Watoto watatu wawafikisha wazazi wao kituo cha Polisi

watoto wakiwa katika michezo ya kila siku
Na mwandishi wetu
Musoma,
WATOTO watatu wa familia moja wamewafikisha wazazi wao katika kituo kikuu cha Polisi Mjini Musoma kitengo cha dawati la jinsia na watoto wakidai kutelekezwa na kuwafanya kuishi maisha ya kutangatanga mitaani ili hali wazazi wao wakiwepo na kuendelea na maisha ya kila siku bila kujua wao wanaishi vipi.
Wakiongea nje ya kituo hicho cha Polisi, mmoja wa watoto hao aliyejitambulisha kwa jina la Justine Kichere amesema baba yao mzazi kwa kushirikiana na mama yao wa kambo ambaye hawakuweza kumtaja jina lake waliwafukuza nyumbani kwa kuwatupia nguo zao kwa kile walichokieleza kudaiwa kuwa (machokoraa) watoto wa mitaani.
Wakielezea chanzo cha tukio hilo la kufukuzwa nyumbani,Justine mwenye umri wa miaka 14 mwanafunzi wa darasa la saba katika shule ya msingi Rwamlimi A iliyopo Manispaa ya Musoma amesema waliitwa na mama yao wa kambo akiwa na wadogo zake wawili James Kichere mwenye umri wa miaka 13 na Gerald kichere mwenye umri wa miaka 12 na kuelezwa kuwa mama yao anaumwa na amelazwa katika hospitali ya Mkoa hivyo kuwataka kwenda kumsalimia mama yao.
Mtoto huyo alieleza kuwa wakiwa njiani kuelekea hospitalini huku wakiwa hawapajui waliomba msaada katika gari moja nakueleza wanakwenda katika hospitali ya Mkoa na kupandishwa kisha kuelekea wasipokujua na walipofika na kuuliza waliambiwa wapo maeneo ya Ramadi.
Alidai baada ya kudaiwa kupotea waliomba msaada wa kurudi nyumbani Musoma na kusaidiwa lakini mara baada ya kufika nyumbani bila kuulizwa kilichowasibu walitupiwa nguo zao nje na kutakiwa kuondoka nyumbani na watafute mahala pengine watakapo kwenda kuishi.
Justine amesema baada ya kufukuzwa na baba yao pamoja na mama yao wa kambo waliamua kwenda kwa mama yao ambaye alitengana na baba yao anayeishi maeneo ya Baruti na kukaa kwa muda wa siku mbili kisha mama yao kuwataka kurudi kwa baba yao kwa kuwaeleza kuwa hana pesa ya kuwalisha wote watatu.
Aliendelea kueleza baada ya kuona hawana sehemu ya kwenda waliamua kutaka kuingia katika maisha ya mtaanii na waliishi katika maisha hayo kwa muda wa wiki moja huku wakiwa wakilala katika jumba bovu maeneo ya Nyakato na kuyaona maisha hayo hawayawezi na kuamua kwenda kituo cha Polisi ili kuweza kupata msaada zaidi.
Mtoto huyo aliongeza kuwa hilo sio tukio la kwanza kwa baba yao Kichere Sangi aliyemueleza kuwa ni mfanyabiashara wa duka la rejareja katika maeneo ya Kigera kufanya hivyo kwa kuwa alishawahi kumfukuza kaka yao Geofrey Kichere aliyekuwa akisoma kidato cha tatu katika shule ya sekondari Bweri ambaye mpaka sasa hajulikani halipo.
Aidha watoto hao wamesema lengo la kwenda katika kituo cha Polisi ni kutaka kupata msaada kwa kuwa maisha wanayoishi mtaani ni magumu na wameshindwa kwenda shuleni huku mmoja wao akiwa anakabiliwa na mtihani wa darasa la saba
BINDA NEWS Ilifika katika ofisi ya dawati la jinsia na watoto katika kituo cha Polisi Musoma kutaka kujua hatima ya watoto hao na kuelezwa kuwa wanazotaarifa hizo na hatua waliyochukua ni kundika barua wa wito kwa wazazi ili kuelezea madai ya watoto hao.

Short URL: http://www.thehabari.com

Mbunge ahukumiwa kifungo au kulipa faini baada ya kupatikana na hatia

Mbunge wa Maswa Mashariki, Sylvester Kasulumbai (CHADEMA), na kada wa chama hicho, Robert William, wamehukumiwa kifungo cha miezi saba jela au kulipa faini ya sh 250,000 baada ya kutiwa hatiani kwa makosa mawili ya jinai.

Adhabu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Tabora, Thomas Simba, muda mfupi baada ya kumwachilia huru mbunge wa Viti Maalum wa chama hicho, Suzan Kiwanga, na mwanachama mwingine, Anwaryn Kashaga.

Kasulumbai na mwenzake walifungwa pingu na kupelekwa katika mahabusu ya mahakama kitendo ambacho kililalamikiwa na wakili Mbogolo kwamba ni cha udhalilishaji na uvunjaji wa haki za binadamu.

“Unakifurahia kitendo unachokifanya? Alisikika Kasulumbai akimuuliza askari polisi aliyemvika pingu mara baada ya hukumu hiyo kutolewa.

Akisoma hukumu ya kesi hiyo, hakimu Simba alisema kuwa hii ni sawa na kesi nyingine zinazowakabili watu wengine kwamba mbunge huyo atakwenda jela miezi mitatu kwa kutoa lugha ya matusi au kulipa faini ya sh 50,000.

Pia aliwahukumu washtakiwa hao kwenda jela miezi minne au kulipa faini ya sh 100,000 baada ya kuwatia hatiani kwa kosa la shambulio liletalo madhara mwilini.

Hakimu Simba vile vile aliwataka washtakiwa hao kumlipa fidia ya sh 2,000,000 mlalamikaji Fatuma Kimario, ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Igunga.

Washtakiwa wote walilipa faini hiyo na kuachiliwa huru huku wakibaki kusubiri kulipa fidia hiyo ya sh milioni moja kila mmoja.

Awali upande wa mashtaka ulidai kuwa washtakiwa wote walitenda makosa hayo Septamba 15 mwaka jana, katika Kijiji cha Isakamaliwa wilaya ya Igunga.

Mara baada ya kuachiliwa huru, Kiwanga na Kashaga walitoka nje na kutimua mbio jambo lililowafanya watu waliokuwepo mahakamani hapo kuwashangaa.

Mapema wakili wa utetezi, Edson Mbogolo, aliiomba mahakama itoe adhabu ndogo kwa wateja wake kwa vile ni wakosaji wa mara ya kwanza na kwamba Kasulumbai (62) ana watoto 27 na wake watatu wanaomtegemea.

“Mahakama izingatie kwamba Kasulumbai ni mwakilishi wa wananchi na endapo akipewa adhabu ya kifungo, jimbo lake litakuwa wazi na hivyo litaigharimu serikali kuitisha upya uchaguzi,” alisema Mbogolo.

Makosa mengine yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa hao ni kumweka chini ya ulinzi isivyo halali kwa mujibu wa sheria Mkuu huyo wa Wilaya, huku kosa la nne ni wizi kutoka maungoni ambalo halikuweza kuthibitishwa na hivyo kufutwa na mahakama.

Kesi ya mauaji Iramba: Dkt. Mkumbo apanda kizimbani na kuunganishwa na wengine 12

Mshauri wa CHADEMA ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Kitila Mkumbo, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya mjini Singida akikabiliwa na tuhuma za kutoa lugha ya matusi kwa mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (CCM).

Dkt. Mkumbo ameunganishwa katika kesi hiyo pamoja na ofisa wa sera na utafiti wa CHADEMA Mwita Mwikwabe (37) ambaye alisomewa pia shitaka hilo Julai 16mwaka huu.

Awali Mwanasheria wa serikali, Maria Mudulugu alidai kwamba Julai 14 mwaka huu, saa 10 jioni, mshtakiwa huyo alitoa lugha ya matusi kwa Mwigulu kuwa ni malaya na mzinzi huku akijua wazi kwamba kitendo hicho ni kinyume cha sheria.

Mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo, Ruth Masamu, mwanasheria huyo alidai kuwa mshtakiwa alitoa lugha hiyo ya matusi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya kituo cha mabasi Kijiji cha Nguvumali, Kata ya Ndago.

Dkt. Mkumbo alikana shitaka hiko na yupo nje kwa dhamana hadi Julai 30 mwaka huu, kesi hiyo itakapotajwa tena.

Nao wakazi wawili wa Kijiji cha Nguvumali, Kata ya Ndago, Paulo Nashokigwa (27) na Emanuel Shila (24), wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya mjini hapa wakikabiliwa na tuhuma za kushiriki kumuuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), Yohana Mpinga (30).

Mwanasheria huyo wa serikali alidai kuwa Julai 14 mwaka huu, saa 10 alasiri katika Kijiji cha Nguvumali, Kata ya Ndago, washtakiwa wote kwa pamoja wakitumia fimbo na mawe, walimpiga Yohana na kumsababishia kifo.

Washtakiwa hao hawakutakiwa kujibu lolote kwa vile Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji. Na wameunganishwa na washtakiwa wengine 12 waliosomewa shitaka lao la mauaji Julai 16 mwaka huu, kesi hiyo itatajwa Julai 30 mwaka huu.

Jumbe za vitisho kwa Nchemba, CHADEMA wasema 'phone spoofing' ilitumika

Ni kweli kuwa katika teknolojia, zipo njia za kufanya telephone spoofing. Zipo huduma za bure (ambazo huambatana na matangazo kila unapotumia huduma hiyo) na ipo huduma ya kulipia ambayo haiambatani na matangazo yoyote. Teknolojia hii si mpya duniani kwani imetumika kwa muda mrefu sana katika nchi zilizoendelea kiasi cha baadhi ya Serikali za nchi hizo kuzuia matumizi yake na kuweka adhabu kali kwa atakayekutikana amekiuka sheria hizo, hii ni kutokana na teknolojia hiyo kutumiwa kufanikisha vitendo vya kihalifu au usumbufu pasina sababu.  Bofya hapa kujielimisha zaidi kuhusu "phone spoofing".
----

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimedai kugundua mbinu zilizotumiwa na mtoto wa kigogo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) za kuingilia mawasiliano ya simu za wabunge wake kutuma ujumbe wa vitisho kwa mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, mjumbe wa Kamati Kuu wa CHADEMA, Mabere Marando, alisema mtoto huyo wa kigogo ambaye hakumtaja jina, alinunua mitambo hiyo kutoka nchini Israel.

Alisema nchini Israeli kuna kampuni mbili alizozitaja kwa majina ya Nice System na Verinty System, ambazo zimefanikiwa kutengeneza mitambo yenye uwezo wa kuingilia mawasiliano ya mtu kwa umbali wa kilometa tano na kwamba moja ya mitambo hiyo ndiyo iliyotumiwa kusambaza ujumbe mfupi wa simu kwa Mwigulu, zikionyesha kuwa zimetoka kwa wabunge wa CHADEMA.

Aliongeza kuwa mfumo uliotumika kuingilia mawasiliano ya wabunge wa CHADEMA unaitwa sms spoofing, na kwamba inaweza kutumiwa na idara za kiusalama kwa sababu maalum tu.

“Tuliwauliza wabunge wetu kama wamefanya suala hilo na wakatuhakikishia kuwa hawahusiki, tukashtuka na kama mshauri wa masuala ya kiusalama wa chama tukaamua kuingia kazini kufuatilia hili, tulichogundua ni kwamba mipango hii iko nyuma ya mtoto wa kigogo wa CCM ni mtaalamu wa mitandao na ana fedha nyingi za kufanyia kazi hii,” alisema Marando.

Alieleza kuwa jambo la kusikitisha ni taarifa walizozipata kuwa mwanasheria mkuu wa serikali Jaji George Werema kuwaagiza watumishi wa ofisi yake kuandaa mashtaka kwa ajili ya tukio hilo la kuwahusisha wabunge wa CHADEMA na meseji hizo badala ya kushughulika na watu walioingilia mawasiliano yao.

Alisema kwa nafasi yake, Werema kama msimamizi mkuu wa sheria nchini anajua wazi kuwa kuingilia mawasiliano ya mtu mwingine ni kosa la jinai na mhusika anayefanya hivyo anapaswa kushtakiwa.

“Kitendo cha Jaji Werema kutoa maagizo ya kuandaa mashtaka kwa wabunge ni kuwasaidia wahalifu; tunachoweza kumuambia ni kwamba taarifa tunazo tutakutana mahakamani kuweka masuala haya wazi,” alisisitiza.

Alisema CHADEMA haitajishughulisha kulifikisha suala hilo mahakamani bali wanasubiri waitwe ili wakaudhihirishie umma namna viongozi wa CCM na watendaji wengine serikalini wanavyotumia vibaya nafasi zao kuwanyamazisha wapinzani wao kisiasa.

Alibainisha kuwa serikali ya CCM isidhani kuwafunga mdomo wakosoaji wake wa sasa ni suluhisho la ushindi kwao kwamba harakati za kudai uhuru wa kweli hazikuanza sasa na hazitaishia kwa kuwadhuru watu.

Wiki iliyopita mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu, alisimama bungeni na kuomba mwongozo wa Spika akidai kuwa amepokea ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa baadhi ya wabunge wa CHADEMA, akitishiwa kuuawa.

Friday, July 20, 2012

Nimrod Mkono atimiza ahadi ya madawati sekondari ya Butuguri


MBUNGE wa Jimbo la Musoma Vijijini Nimroadi Mkono amekamilisha ahadi yake ya kupeleka Madawati mapya katika shule ya sekondari Butuguri baada ya kubainika kuwa madawati yaliyotengenezwa na mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF katika shule hiyo hayana ubora.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kupokea awamu ya kwanza ya Madawati zaidi ya 50,diwani wa kata ya Butuguri Mwita Charles alimpongeza Mbunge huyo kwa kukamilisha ahadi hiyo huku akitoa wito kwa viongozi wengine kuiga mfano huo.
Diwani huyo alisema kuwa Madawati yaliyotengenezwa na TASAF hayana ubora na hivyo anaunga mkono kauli ya Mh Mbunge kuyarudisha Madawati hayo katika Halmashauri ya Musoma.
Kuhusu wale wote waliohusika katika ubadhilifu huo diwani huyo alisema kuwa wanatakiwa kuchukuliwa hatua za kisheria ili iwe fundisho kwa viongozi wengine ambao wapo kwa masilahi yao.
Naye Mwalimu mkuu Wa Shule hiyo Godfrey Robert alisemshukuru Mbunge huyo na kusema kuwa amesaidia kupunguza mzigo kwa wazazi katika kukabiliana na upungufu wa madawati uliokuwepo shuleni hapo.
Amesema Madawati yaliyokuwepo hayatoshi ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi waliopo katika shule hiyo,na hivyo mwaka huu walikuwa na mpango wa kutengeneza madawati hayo.
Aidha madawati yote yaliyotengenezwa na mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF tayari yamerudishwa katika halmashauri ya Musoma Vijijini kutokana na kutokuwa na kiwango kinachokubalika
Hivi karibuni akifanya ziara shuleni hapo mbunge wa jimbo la Musoma Vijijini Nimrodi Mkono aliyakataa madawati zaidi ya 1000 yaliyotengenezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF kutokana na kutokuwa na kiwango chenye ubora

Orodha yenye baadhi ya majina ya marehemu wa ajali ya MV Skagit

Jeshi la Polisi nchini, limetangaza orodha ya majina ya watu waliofariki katika ajali ya meli ya MV Skagit, iliyotokea juzi katika eneo la Chumbe Kisiwani Zanzibar.

Licha ya kutaja majina hayo, idadi ya miili ambayo hadi jana imepatikana kutokana na kazi kubwa ya uokoaji inayofanywa na Vikosi vya Ulinzi na Usalama, imefikia watu 63. Kati ya watu hao, waliopatikana na idadi kwenye mabano ni pamoja na wanawake (41), wanaume (9) na watoto (12), ambapo kati yao wakiume ni (5) na wa kike (7).

Msemaji wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Mohammed Muhina, alitaja baadhi ya majina ya marehemu waliotambuliwa kuwa ni:

  1. Mwanahamisi Mshauri Maneno (42, Kibanda Maiti Zanzibar)
  2. Maua Ramadhan Feruzi (29, Mwembeladu)
  3. Khadija Omari Ally (58), Kimahewa)
  4. Mgeni Juma Khalifa (25, Daraja Bovu)
  5. Amina Ahmed Ramadhan (21, Bumbi Matola, Michenzani)
  6. Khadija Othuman Juma (50, Michenzani)
  7. Mohammed Said Salum (42, Magomeni Mikumi, Dar es Salaam)
  8. Khadija Rajab Kibune (22, Fuoni)
  9. Hussein Ally Khamis (miaka 4, Mwanakwerekwe)
  10. Nas Victor Kadozo (30 Mbagala Rangi Tatu, Dar es Salaam)
  11. Anita Emanuel (42, Kibamba, Dar es Salaam)
  12. Rukiya Issa Muombwa (miezi 2, Meli Nne Fuoni)
  13. Halima Ali Khamis (23, Mtopepo)
  14. Kolin Krispin (miezi 9, Kunduchi, Dar es Salaam) 
  15. Rahma Ali Abdallah (52, Mfenesini, Zanzibar)
  16. Said Jumanne Masanja (9, Nzega, Tabora)
  17. Sauda Abdallah Omar (22, Ole, Pemba)
  18. Said Juma Said (36, Arusha)
  19. Amina Abdallah Tindwa, (miezi 6, Fuoni)
  20. Halima Ramadhani Kilimo, (53, Morogoro)
  21. Amina Hamir Bakari (39, Chukwani)
  22. Ali Hamdu Othman (35, Mkwajuni) 
  23. Sabiha Heri Mbarouk (25, Mgeleme, Chakechake Pemba)
  24. Halima Ali Mohamed (35, Kiwengwa)
  25. Asia Juma Khamis (29, Kiembe Samaki)
  26. Yusuf Hassan Yusuf (7, Chamazi, Dar es Salaam)
  27. Batuli Abdulrahman Amir (20, Jang’ombe)
  28. Fatma Said Sultani (54, Msasani Dar es Salaam)
  29. Juma Jafari Shajak (miezi 6, Tanga)
  30. Mohamed Ali Ngombe (41, Buguruni, Dar es Salaam)

Wednesday, July 18, 2012

Wazazi watakiwa kujipanga katika malezi


WAZAZI wametakiwa kuwalea watoto katika maadili mema pamoja na kuwajengea misingi imara ya kielimu kutokana na ukweli kwamba elimu ndio urithi kipekee ambao mzazi anaweza kumwachia mwanae.
Rai hiyo ilitolewa na vijana wa kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT)Dayosisi ya Kaskazini usharika wa Moshi Pasua, wakati wa kufunga juma la vijana ambalo huadhimishwa mwezi julai kila mwaka.
Vijana hao walisema ni jukumu la kila mzazi kuhakikisha anatimiza wajibu wake wa malezi bora kwa watoto ikiwemo kuwapatia elimu, hatua ambayo itawawezesha kukabiliana na changamoto za kimaisha pindi watakapofikia kujitegemea.
Akizungumza Bw. Nimrod Kimaro alisema kuwajengea watoto misingi thabiti ya elimu huwafanya kuwa imara na kujiamini hivyo kuongeza idadi ya wasomi hapa nchini na kupunguza tatizo la watoto wa mitaani ambalo kwa kiasi kikubwa linachangiwa na mimba zisizotarajiwa.
Bw. Kimaro alisema kumekuwepo na wazazi wengi ambao wamebweteka katika malezi, hali ambayo inachangia vijana kuharibikiwa kimaisha ikiwa ni pamoja na kuijiingiza katika vitendo viovu ikiwemo uvutaji wa madawa ya Kulevya na Ngono zembe.
“Wazazi wengi wamekuwa chanzo cha sisi vijana kuharibikiwa kimaisha kwani wamejisahau katika malezi na hali hii inasababisha kuwepo kwa kundi la vijana lisilo la maadili ambako ndiko kunapatikana vibaka,wezi na walevi wa kupindukia na baada ya hapo mimba za zisizotarajiwa,mimba za utotoni na hata maambukizi ya ugonjwa hatari wa ukimwi”alisema Kimaro..
Alisema ni vema wazazi wakajijengea tabia ya kuwa karibu na watoto
wao ili kuweza kuwaepushia matatizo ambayo hukumbana nayo pindi wawapo
mashuleni kwa madai kuwa watoto wengi hupoteza mwelekeo wa kimaisha
kutokana na wazazi wao kutojipanga vizuri katika malezi.
Akizungumza katika kilele hicho cha juma la vijana mchungaji kiongozi wa Usharika wa Moshi Pasua Bw. Elirehema Silaa aliwataka vijana kujitambua na kujijengea tabia ya kujishughulisha na kazi mbalimbali za kimaendeleo hatua ambayo itawasaidia kuondokana na hali ya utegemezi katika jamii.

Tuesday, July 3, 2012

Serikali itazame upya mfumo wa ufundishaji



Na mwandishi wetu
SERIKALI imeshauriwa kutizama upya sera ya elimu na kubadili mfumo wa ufundishaji mashuleni hatua ambayo itasaidia kukabiliana na tatizo la ongezeko la watoto wanaomaliza elimu ya msingi huku wakiwa hawajui kusoma wala kuandika.
Ushauri huo ulitolewa jana na ASkofu wa kanisa la kiinjili la kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Dkt.Martine Shao wakati akifungua kongamano la walimu wa shule na vyuo vya Montesori kutoka mikoa yote ya Tanzania lililofanyika mjini moshi ambapo alisema ongezeko la wanafunzi kumaliza elimu ya msingu huku wakiwa hawajui kusoma na kuandika linazidi kurudisha nyuma kiwango cha elimu hapa nchini.
Alisema wanafunzi kumaliza elimu ya msingi wakiwa hawajui kusoma na kuandika inatokana na mazingira yasiyo mazuri katika shule za serikali kuanzia ngazi za awali hadi sekondari hivyo umefika wakati sasa kwa serikili kutafuta njia ya kukabili tatizo hilo kabla halijaleta madhara makubwa.
“Ni wakati sasa kwa serikali kutazama suala la elimu kwa upya kwani taarifa za wanafunzi kumaliza elimu ya msingi huku wakiwa hawajui kusoma na kuandika zinaumiza sana kwani jambo hili haliwaingii watu wengi akilini kwamba mwanafunzi amesoma miaka saba na ametumia fedha nyingi za wazazi halafu anamaliza hajui kusoma,kuandika wala kuesabu hii ni hatari sana kwa hapo baadae na ni lazima serikali itafute suluu mara moja”alisema Dkt. Shao.
Aidha Dkt. Shao alisema ni vema serikali ikaona umuhimu wa kuwekeza katika elimu kutokana na kwamba katika nchini ya Tanzania kumekuwepo na rasilimali nyingi ambazo zimekuwa zikitumiwa na watu wachache kujinufaisha binafsi ili hali shule za serikali hazina vifaa vya kufundishia, walimu wa kutosha wala maabara licha ya serikali kusema inataka kuinua kiwango cha sayansi.
Dkt. Shao alisema Tanzania imekuwa ikitumia fedha nyingi kwa mambo yasiyo na maana na kwamba endapo raslimali za nchi kama madini yangetumika vizuri na kuona umuhimu wa elimu wanafunzi mashuleni wasingekosa madawati,vitabu , walimu wa kufundisha wala maabara.
Katika hatua nyingine Askofu shao alisema hali iliyopo sasa ya ufisadi,rushwa, dhuluma na ukatili katika taifa inatokana na watanzania kutokuwa na maadili hivyo ni vema watoto wakaandaliwa vizuri toka katika shule za awali ili kuweza kumaliza matatizo hayo.
Nao baadhi ya walimu walioshiriki katika kongamano hilo walisema wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mishahara midogo pamoja na wao kutothaminiwa hivyo kuiomba serikli kuona umuhimu wa kuwaajiri na kuwalipa stahiki zao kama watumishi wengine hapa nchini.

Bodi ya Wadhamini Muhimbili yatoa masharti makali kwa madaktari



Wauguzi Hospitali ya Muhimbili
*Yawataka madaktari warejee kazini, mwisho Julai 3
BODI ya Wadhamini ya Hospitali ya Taifa Muhimbili imekutana na kutoa maagizo makali kwa uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kuhusiana na mgomo wa madaktari unaoendelea nchini kote.
Bodi hiyo iliyokutana tanu Juni 28, 2012 imewataka madaktari waliogoma warejee kazini mara moja kutii amri ya Mahakama Kuu Kitengo cha kazi, kwa mujibu wa Kifungu Na. 76 (1) na (2) cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini ya mwaka 2004, kabla ya uongozi wa hospitali hiyo kutoa adhabu.
Katika taarifa yao kwa uongozi wa Muhimbili, iliyosainiwa na Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Dk. Gabriel Upunda; Bodi imeutaka uongozi kuwachukulia hatua za kinidhamu wafanyakazi wote watakaoendelea na mgomo wakiwemo baadhi yao wanaohudhuria kazini na kutofanya kazi bila sababu za msingi jambo ambalo ni kinyume na taratibu za kazi.
Bodi hiyo iliyokutana kujadili na kutathmini hali ya utendaji na utoaji wa huduma hivi sasa katika Hospitali ya Muhimbili imewataka madaktari wote waliopo likizo warejee kazini mara moja, huku ikidai tayari utaratibu wa kufidia likizo na nauli umeandaliwa.
“…Uongozi wa Hospitali uwachukulie hatua za kinidhamu wafanyakazi wote watakaoendelea kutokuhudhuria kazini na kufanya kazi bila sababu za msingi kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na taratibu za kazi; Uongozi wa Hospitali ufute mara moja ‘rotations’ za Madaktari waliopo kwenye mafunzo kwa vitendo (interns),” ilieleza taarifa hiyo.
Tayari uongozi wa Muhimbili umetoa tangazo kwa madaktari wote kutekeleza maelekezo ya bodi huku ikielekeza madaktari kujiorodhesha kwa wakuu wa vitengo na mwisho wa zoezi hilo ni kesho Julai 3, 2012 saa tatu asubui. Baada ya muda huo kwa madaktari ambao wataendelea na mgomo watachukuliwa hatua za kinidhamu.

Ni miaka 20 tangu kutungwa sheria kuruhusu Vyama Vingi; Bado upinzani ni sawa na uadui!

Ndugu zangu, 

Tarehe kama ya leo miaka 20 iliyopita, yaani tarehe 2 Julai, 1992, Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha sheria ya kuruhusu kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi. 

Miaka 20 imetimu, tumepiga hatua, lakini, mpaka hii leo, bado upinzani kwa wengine unatafsiriwa kama ni uadui, na wakati mwingine ni uhaini. 

Na katika Tanzania yetu, wenye fikra za kukipinga Chama tawala, CCM na Serikali wamekuwa wakitengwa na hata kupewa majina mabaya. Nimeshawahi kumsikia mtu akiambiwa;

“Alaa, unaongea na Lipinzani hilo!” Kana kwamba aliyeitwa ‘ Lipinzani’ hakuwa Mtanzania na binadamu kama wengine.

Na hakika, katika kujadili hili la Katiba Mpya, tuna kila sababu ya kuipitia historia yetu. Maana, naamini, kuwa historia ni mwalimu mzuri. 

Itakumbukwa, katikati ya vuguvugu lile la mageuzi ya kisiasa miaka ya 90 mwanzoni, Watanzania zikatufikia habari; kuwa Oscar Kambona, aliyekosana na Nyerere na aliyekimbila uhamishoni Uingereza, alikuwa njiani kurudi nyumbani. Ujio wa Oscar Kambona ukawa gumzo la mjini na nje ya jiji. Kuna waliojiandaa kwenda uwanjani kumpokea.

Usiku mmoja ikasikika sauti ya Bw. Mrema redioni. Sauti ya Waziri wa Mambo ya Ndani. Mrema alitamka, kuwa kama Kambona angekanyaga mguu wake Dar es Salaam, basi, angekamatwa kujibu mashtaka ya uhaini.

Ni hofu ile ile ya Serikali hata wakati huo. Hofu ya kuimarika kwa fikra za upinzani na kukua kwa upinzani. Mrema akatumika au akajituma kuwatisha na kuwakatisha tamaa Watanzania. Kambona alikanyaga Dar, hakuwa na mashtaka ya kujibu. Ulikuwa ’ mkwara’ tu, kama wanavyosema mitaani.

Na Mrema, akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, aliifanya kweli kazi ya kuwa ’ Mbwa wa Serikali’. Alibwaka kweli kweli. Nakumbuka usiku mmoja mwanzoni mwa miaka ya tisini nilimsikia Mrema akiongea redioni kutishia maandamano ya CUF. Maandamano yale yalikuwa yahitimishwe kwa mkutano viwanja vya Mnazi Mmoja. Mwenyekiti wa CUF, Bw. James Mapalala ndiye alikuwa aongoze maandamano hayo na kuhutubia.

Augustino Lyatonga Mrema akaaunguruma redioni usiku ule. Alishusha ’ mkwara’ mzito. Kuwa maandamano hayo si halali na yangekutana na nguvu za dola. Kesho yake, CUF waliingia mitaani. Ndio, Ungangari wa CUF ulianza siku nyingi.

Pale Mnazi mmoja FFU wakamwagwa, na farasi wao pia. Virungu vilitembea. James Mapalala, Mwenyekiti wa CUF, hakuonekana. Kukawa na taarifa, kuwa anatafutwa na polisi.

Dar ilikuwa ndogo wakati huo, lakini James Mapalala hakupatikana .
Ninazo taarifa za kuaminika za Kibalozi, kuwa James Mapalala alikuwa amejificha kwenye moja ya makazi ya rafiki yake, balozi wa nchi moja ya Kimagharibi. Ni balozi gani huyo? Na nini hasa kilitokea miaka 20 iliyopita?

James Mapalala yungali hai. Huu ni wakati kwa waandishi vijana kuwatafuta wazee veterani wa harakati za mageuzi ya kisiasa hapa nchini. Wazee kama akina James Mapalala.

Hawa ni watu muhimu sana watakaotusaidia kupokea simulizi zao. Kisha ziwekwe kwenye maandishi, na iwe kumbukumbu za kihistoria. Ni historia yetu, tusiionee aibu. Ni urithi tutakaowaachia wajukuu zetu ili nao waweze kujifunza. Waweze kujitambua na kujenga mioyo ya uzalendo.

Maggid Mjengwa, 
Barcelona, Spain
mjengwablog.com