Wednesday, July 25, 2012

Farijara Hussein; Rajabu Maranda wamehukumiwa kufungo cha miaka 3

KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rajabu Maranda na ndugu yake, Farijala Hussein, wamehukumiwa kifungo cha miaka 18 jela, baada ya kukutwa na hatia katika makosa sita, yakiwemo ya kujipatia Sh bilioni 2.2 kutoka katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), iliyopo Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Washitakiwa wamehukumiwa kifungo cha miaka mitatu kwa kila kosa kwa makosa sita, lakini adhabu hiyo inakwenda kwa pamoja kwa hivyo watatumikia miaka 3 tu.

Washitakiwa hao, walitiwa hatiani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na jopo la mahakimu watatu, Projest Kahyoza, Fatuma Masengi na Catherine Revocath.

Mahakimu hao, walitofautiana katika uamuzi, hali iliyosababisha kuandaa hukumu mbili, moja iliandaliwa na mahakimu wawili, Kahyoza na Revocath na hukumu ya pili, iliandaliwa na Masengi.

Hukumu iliyoandikwa na mahakimu wawili ndiyo inayochukuliwa kuwa ya mahakama, ambayo imewatia hatiani washitakiwa hao na hukumu ya Masengi iliwaachia huru washitakiwa wote kwa madai upande wa mashitaka, ulishindwa kuthibitisha mashitaka bila kuacha shaka.

Akisoma hukumu ya kwanza, Kahyoza alisema washitakiwa walikuwa wanakabiliwa na makosa saba ya kula njama, kughushi, kutoa nyaraka za uongo, kughushi, kutoa tena nyaraka za uongo, wizi na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

“Katika mashitaka ya kughushi, hakuna shaka kwamba upande wa mashitaka waliweza kuthibitisha kosa, kwani waliokuwa wakidaiwa kuwa wamiliki halali wa Kampuni ya Money Planner & Consultant, hawajawahi kuwepo ni wa kufikirika.

“Washitakiwa walitumia majina hayo kwa udanganyifu, wakionyesha kwamba waliteuliwa kuiwakilisha Kampuni ya Kijerumani, B. Grancel kudai madeni BoT wakati si kweli,” alisema.

Alisema washitakiwa hakuna shaka kwamba walighushi hati iliyokuwa ikiwaruhusu kuchukua fedha za kampuni hiyo na kwamba taratibu zilifuatwa na waliwekewa kiasi cha fedha katika akaunti yao, iliyokuwepo Benki ya Biashara Afrika.

Alisema nyaraka za kuomba kulipwa kiasi hicho, zilikaguliwa na viongozi mbalimbali wa BoT na kuona zilikuwa sahihi bila kubaini zimesainiwa na upande mmoja wa Kampuni ya B. Grancel.

“Hati zilikuwa zimesainiwa na Jonath wa Kampuni Grancel ya Ujerumani, lakini Fundi Kitunga na Paul Thobias wa Kampuni ya Monney Planner hawakusaini.”

Upande wa mashitaka, umeweza kuthibitisha washitakiwa walitumia hati za kughushi kuchukua fedha BoT na shitaka la saba la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu limethibitika, kwani nyaraka za kughushi zilitumika na shtaka hilo lilishathibitika pia.

Pia upande wa mashitaka, uliweza kuthibitisha bila kuacha shaka kwamba, washitakiwa walikula njama na walishindwa kuthibitisha bila kuacha shaka katika shtaka la sita kwamba waliiba Sh 660,210,000.

Alisema wakiachia mbali shtaka la sita, washitakiwa wanatiwa hatiani katika mashtaka yote sita yaliyobaki kutokana na upande wa mashitaka kuthibitisha, bila kuacha shaka kwamba walitenda makosa hayo kwa nia mbaya.

Alisema hakuna ushahidi uliotolewa mahakamani na upande wa mashitaka ukionyesha kwamba Kampuni ya Kijerumani ya Gransel haikuwepo, haikuwa inaidai BoT na wala haikuwaruhusu Kampuni ya Money Planner kudai madeni yao.

Akisoma adhabu, Hakimu Revocath alisema washitakiwa wanahukumiwa kutumikia kifungo cha miaka mitatu katika kila kosa kwa makosa sita, lakini adhabu hiyo inakwenda kwa pamoja, “Washitakiwa watatumikia kifugo cha miaka mitatu mitatu kwa kila kosa, adhabu itakwenda kwa pamoja na inaanza leo (jana),”alisema Revocath na kuongeza adhabu hiyo kwa kosa la kwanza, pili, tatu, nne, tano na saba.

No comments:

Post a Comment