Tuesday, May 29, 2012

Ezekiel Maige: Chama Cha Mapinduzi kitakufa na kujizika chenyewe

 

picha Ezekiel Maige na mwananchi
Mwananchi wa Mjini Kahama, Mkoani Shinyanga, Bw. Marco Kanjiwa, akilia wakati wa mapokezi ya Mbunge wa Jimbo la Msalala Bw. Ezekiel Maige (kulia), baada ya kufika eneo hilo kwa mara ya kwanza jana, tangu alipovuliwa Uwaziri wa Maliasili na Utalii. Mapokezi ya Mbunge huyo yameghubikwa na vilio na simanzi kutoka kwa wapiga kura wake. (picha: Nyakasagani Masenza)
Aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Bw. Ezekiel Maige ameibuka Mjini Kahama leo na  kueleza kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM) kisipokuwa makini kukomesha makundi, fitina, majungu na chuki binafsi, kitakufa na kunajizika chenyewe.

Maige aliyasema hayo leo asubuhi alipozungumza kwenye ofisi ya CCM ya mjini Kahama, alipokuwa akiongea na Viongozi wa chama hicho baada ya kuzunguka kwenye jimbo la Msalala na kusema makundi, fitina, chuki na majungu ya kipumbavu yatasababisha chama hicho kipoteze mwelekeo.

Mbele ya Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Shinyanga Bw. Hamis Mgeja,  Bw. Maige amesema, ndani ya CCM imeibuka tabia mbaya ya  kushabikia majungu ya kipumbavu, badala ya kushughulikia kero za Wananchi. 

"Kitendo cha baadhi ya wanachama wa CCM kushabikia kuondolewa kwangu kwenye nafasi ya Uwaziri ni imeonyesha ujinga wa kisiasa wakidhani kuwa wanamkomoa Maige kumbe wanakikomoa chama na kukiweka katika mazingira magumu katika jimbo langu la Msalala, kwa sababu ubunge wangi unaifanya CCM iweze kulipwa ruzuku inayofanya watendaji wake kulipwa mishahara zinatokana na kuwepo kwangu kwenye jimbo hili," alisema Maige.

Alisema CCM pamoja na kuwa na nyezo zote gari, pikipiki lakini hajafanya hata mkutano hata mmoja kwenye  jimbo lakini CHADEMA  wasiokuwa hata na baiskeli wameweza kupita jimbo zima wakifanya mikutano yao na kugawa bendera, kadi zao kwa imani kuwa kuondolewa kwake katika nafasi ya Uwaziri ni kama ushindi kwao

Alisema wanachama na wapenzi wake wako katika hali tete wakimtaka awaeleze anahama wapi lakini anawatuliza na kuwapa  pole kwa yaliyomfika ya kuzushiwa tuhuma kwenye Wizara kwa lengo la kumchafua na kupelekea kuwajibishwa.
  
Aidha katika kikao hicho cha kueleza yaliyojiri Bungeni  alizungumzia  Kamati inayoongozwa na mwenyekiti Bw. James Lembeli ya Ardhi, Maliasili na Mazingira alisema taarifa yake rasmi haiendani na taarifa iliyosomwa bungeni hali ambayo alidai ilikuwa na tuhuma za uongo zilizojaa chuki, fitina kwa lengo la kumng’oa kwenye Uwaziri.

Bw. Maige amemtaka Mbunge Lembeli kwa kuwa ametekeleza lengo lake la kumng’oa kwenye Uwaziri, warudi mezani kwenye mazungumzo yenye kuwaletea maendeleo wananchi  kwa vile majimbo yao yote yako wilaya moja ya Kahama na kabla ya kupata wadhifa huo walikuwa marafiki na walitembea pamoja kwenye majimbo yote ya Kahama na Msalala kwenye mikutano yao lakini alipopata Uwaziri walichukiana.

Naye Katibu Msaidizi wa CCM Wilaya ya Kahama, Bw. Hamadi Masoud alisema suala la ugomvi na uhasama walionao Wabunge hao wa Msalala na Kahama litafikishwa kwenye Kamati ya Maadili ya chama ili liweze kufanyiwa kazi na kuweza kutatuliwa kwa kufaata vikao hivyo.

Katibu huyo Msaidizi  alitoa kauli hiyo baada ya Bw. Maige kueleza kuwa anashangaa na kitendo cha Bw. Lembeli kumpiga vita hali iliyopelekea kumung’oa katika nafasi ya Uwaziri sasa  amefukuzwa kwanini  tena anaendeleza majungu, chuki, fitina ambapo sasa ni Mbunge kama yeye?

Kwa upande wake  Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Bw. Hamis Mgeja alisema maamuzi ya Rais Jakaya Kikwete wananchi wa Kahama hawawezi kuyapinga  kwa madai nafasi hizo unapoteuliwa huwezi kuhoji na unapofukuzwa napo pia huwezi kuhoji  lakini kuichezea nafasi  kwa majungu na fitina zisizo na ukweli ni ujinga  kwa watu wasiopenda maendeleo.

Nyakasagani Masenza
nyakasagani.blogspot.com 

No comments:

Post a Comment