Wednesday, May 30, 2012

Mawaziri waliotemwa waingizwa Kamati za Bunge

WALIOKUWA mawaziri katika Baraza la Mawaziri lililopanguliwa na kusukwa upya hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete na kubaki na ubunge, wamepangwa rasmi kwenye Kamati za Kudumu za Bunge.

Kwa mujibu wa Spika wa Bunge, Anne Makinda, aliyekuwa Waziri wa Fedha Mustafa Mkulo amepangiwa Kamati ya Maendeleo ya Jamii huku aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja akaingizwa kwenye Kamati ya Sheria Ndogo na aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige (Fedha na Uchumi).

Wengine ni aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara Dk Cyril Chami (Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), aliyekuwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk Hadji Mponda (Katiba, Sheria na Utawala) na aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi Omary Nundu (Viwanda na Biashara).

Aidha, Makinda amewapangia kamati waliokuwa naibu mawaziri ambao ni Dk Lucy Nkya aliyekuwa Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii (Kilimo, Mifugo na Maji) na Athuman Mfutakamba aliyekuwa Naibu Waziri wa Uchukuzi (Nishati na Madini).

Pia Spika amempangia Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema) na Mbunge wa Viti Maalumu, Subira Mgalu (CCM), amepangiwa Kamati mpya ya Fedha na Uchumi kutoka Kamati ya awali ya LAAC.

Mgalu ameondolewa LAAC kwa kuwa sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Muheza ambapo kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge kifungu namba 113 (2), hairuhusiwi kwa mjumbe wa kamati hiyo kuhusika moja kwa moja na halmashauri, jambo ambalo litakuwa ni mgongano wa maslahi. Aidha, kamati tatu za Bunge ambazo ni Fedha na Uchumi, Sheria Ndogo na Nishati na Madini zinatarajiwa leo kuchagua wenyeviti wake wapya kutokana na waliokuwapo awali kuteuliwa kuwa mawaziri.

Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi, Dk Abdallah Kigoda ameteuliwa kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, George Simbachawene wa Sheria Ndogo amekuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini na wa Nishati na Madini, January Makamba sasa ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia.

Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, James Mbatia hajapangiwa kamati hadi atakapoapishwa katika Bunge.

No comments:

Post a Comment